Ruto amshambulia Orengo, amtaka aache kuwa ‘kibaraka wa Uhuru’, ajiunge na serikali
KATIKA siku yake ya tatu ya ziara ya Nyanza, Rais William Ruto alipeleka mapambano yake ya kisiasa dhidi ya vuguvugu la Linda Mwananchi hadi Siaya, ngome ya Gavana James Orengo, akiwataka wapigakura kukataa vyama vipya ambavyo alisema havijathibitisha uwezo wao wa kuongoza nchi.
Rais Ruto aliwataka wakazi kuunga mkono vyama vilivyo katika serikali jumuishi, akipuuza vyama vipya ambavyo bado havijasajiliwa rasmi.
Alisema vyama hivyo havina uzoefu, mtandao wa kitaifa wala mipango thabiti ya kuongoza Kenya.
Ziara yake Siaya ilikuwa na umuhimu wa kisiasa, hasa kwa kuwa viongozi wa Linda Mwananchi wanatarajiwa kuzuru eneo hilo siku chache zijazo.
Rais Ruto pia alimshambulia Gavana Orengo kwa kuhusishwa na vuguvugu hilo, akimtaka badala yake kushirikiana na serikali katika kuleta maendeleo Siaya.
“Namwambia Orengo aache kundi hilo linaloitwa Linda Sponsors au Linda Sponyo na ajiunge nami katika safari hii ya maendeleo na kujenga hospitali. Je, ninyi watu mlimchagua ajiunge na Linda Sponsors? Kwa nini anaruhusu kuwa kibaraka wa kisiasa na kutumiwa na rais mstaafu?” Rais Ruto alisema.
Pia alimshambulia Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, akimlaumu kwa kuacha jukumu la kuwa kiongozi mstaafu na kuingia katika siasa za upinzani dhidi ya serikali yake.
Rais Ruto alisema Bw Kenyatta alikuwa akiwafadhili wanasiasa wanaompinga baada ya kushindwa kutekeleza baadhi ya mipango aliyokuwa nayo katika sekta ya elimu na afya.
Akizungumza alipokuwa akikagua ujenzi wa Daraja la Dhogoye, Siaya, Rais Ruto aliunganisha ujumbe wa maendeleo na siasa, akisema serikali jumuishi imefungua ukurasa mpya wa maendeleo katika Nyanza.
“Serikali jumuishi ndiyo muungano pekee wenye uwezo wa kuunganisha taifa letu. Ndiyo yenye historia ya utekelezaji, maono ya kuaminika ya siku zijazo na mpango wa kushughulikia changamoto zinazokabili taifa,” alisema.
Alionya wapigakura dhidi ya kuunga mkono vyama vipya, akisema Kenya haiwezi “kujaribu” viongozi wasio na historia ya utekelezaji.
“Taifa letu halitajaribu watu wanaofanya majaribio. Msicheze kamari na watu ambao hawana mpango au historia ya wazi ya kuwafanyia kazi wananchi,” alisema.
Rais Ruto pia alimwalika Mbunge wa Ugenya David Ochieng, ambaye anaongoza chama cha Movement for Democracy and Growth (MDG), kujiunga na serikali jumuishi.
Bw Ochieng alikubali ombi hilo, lakini akaomba Rais Ruto kumuunga mkono katika azma yake ya kumrithi Bw Orengo kama Gavana wa Siaya.
Aliahidi kumpa Rais Ruto asilimia 99.9 ya kura za Ugenya katika uchaguzi wa 2027 iwapo atapata uungwaji mkono huo.
“Nimefurahia kufanya kazi nawe, Mheshimiwa Rais, kwa sababu umekuwa rafiki mzuri. Umetusaidia kuendeleza Ugenya… ndiyo maana tutakupa asilimia 99.9 ya kura zetu,” alisema Bw Ochieng.
Viongozi walioandamana na Rais Ruto walitumia ziara hiyo kumshambulia Gavana Orengo, ambaye hakuwa kwenye ziara hiyo.
Waziri wa Kawi na Petroli Opiyo Wandayi alisema viongozi wengi wa Siaya wameungana isipokuwa mmoja, akimtaja Bw Orengo.
“Rais Ruto, tuachie Orengo sisi. Tutahakikisha anaenda nyumbani,” alisema Bw Wandayi.
Gavana wa Homa Bay na Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga pia alimshambulia Bw Orengo, akimtaka aache kupotosha jamii ya Luo.
Naibu Gavana wa Siaya William Oduol alijitangaza kuwa kaimu gavana kutokana na kutohudhuria kwa Bw Orengo.
Rais Ruto alitaja miradi kadhaa ya maendeleo ambayo serikali imepanga kutekeleza Siaya.
Alisema ujenzi wa barabara ya kilomita 500 inayozunguka Ziwa Victoria utaanza Novemba 2026, baada ya kusubiriwa kwa zaidi ya miaka 15.
Barabara hiyo itaunganisha Busia na Muhuru Bay kaunti ya Migori kupitia Siaya, Kisumu na Homa Bay.
Aidha, Sh32 bilioni zitatumika kujenga kilomita 400 za barabara mpya Siaya.
Rais Ruto pia alisema Sh10 bilioni zimetengwa kwa uchumi wa baharini, ikiwemo utafiti na teknolojia ya uzalishaji wa samaki wachanga, gati nne, huduma za feri na vituo vya uokoaji.