• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Pesa zinazonyang’anywa wafisadi zitumike kulipa madeni – Ole Sapit

Pesa zinazonyang’anywa wafisadi zitumike kulipa madeni – Ole Sapit

Na Mwandishi Wetu

KIONGOZI wa Kanisa la Kianglikana Nchini (ACK) Askofu Mkuu Jackson Ole Sapit ameishauri serikali kutumia pesa na mali inazotwaa kutokana na vita dhidi ya ufisadi kulipia madeni ya kigeni.

Alisema kuwa kanisa hilo linaunga mkono juhudi za serikali kupigana na uovu huo na akahimiza asasi zilizotwikwa jukumu la kuchunguza kesi za ufisadi zipewe nafasi ya kuendesha shughuli hiyo bila kuingiliwa.

Ole Sapit alikuwa akiongea katika eneo la Badasa katika kaunti ndogo ya Marsabit mnamo Ijumaa alipoweka jiwe la msingi kwa ujenzi wa Shule ya Upili ya Wavulana ya St Andrews.

Askofu huyo Mkuu alisema kuwa Kenya inadaiwa deni kubwa na mataifa ya kigeni na hivyo itakuwa jambo la busara ikiwa sehemu ya pesa zilizokombolewa kutoka kwa wafisadi zitatumiwa kulipa madeni hayo.

Kiongozi huyo wa ACK alionya wanasiasa dhidi ya kuingiza siasa katika vita dhidi ya jinamizi hilo akisema kuwa Tume ya EACC na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) zinahitaji mazingira faafu kuwakamata wahusika.

 

You can share this post!

Mpuuzeni Orengo kumpangia Ruto mabaya – Raila

Wafungwa wamlilia Rais awaachilie

adminleo