• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Lahaja za Kiswahili na maeneo zinakozungumzwa

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Lahaja za Kiswahili na maeneo zinakozungumzwa

Na MARY WANGARI

KISWAHILI ni lugha inayosheheni lahaja chungu nzima.

Japo wataalamu hawajaafikiana kuhusu idadi kamili ya lahaja zenyewe na mipaka yake,wengi wao wanakubaliana kwamba kuna lahaja zaidi ya kumi na tano.

Baadhi ya lahaja hizo kwa kurejelea maeneo zinakozungumzwa ni kama zifuatazo:

LAHAJA ZA KASKAZINI

KIAMU

Ni lahaja inayozungumzwa kwenye kisiwa cha Lamu ambacho zamani kilifahamika kama Amu. Kiamu ni lahaja ambayo, sawa na Kimvita,inatumiwa sana katika tungo nyingi za zamani za ushairi. Lahaja ya Lamu ina sifa ile ile sawa na Kimvita ya kutumia sauti ‘t’ badala ya ‘ch’. Sifa nyingineya lahaja hii ni sauti ‘g’ na ‘l’ kudondoshwa inapotokea baina ya irabu au sauti za irabu.

Tazama mifano ifuatayo:

KIAMU KISWAHILI SANIFU
ndia njia
mbegu mbeu
Kiyakazi kijakazi
nduu ndugu
Mbele mbee

KIPATE

Hii ni lahaja ya Kiswahili inayozungumwa katika kisiwa cha Pate.

Ni lahaja ambayo pia inatumiwa sana katika maandishi mengi hasa ushairi wa zamani.

Katika lahaja hii, sauti ‘th’ hutumiwa katika maneno ambayo yana sauti ‘z’,‘dh’ au hata ‘v’ katika Kiswahili sanifu.

Kwa mfano:

KIPATE KISWAHILI SANIFU
Baratha baraza
Uthia Udhia
Muhuwa Marehemu
Pija Piga
Kondo Vita

KISIU

Hii ni lahaja ambayo hutumiwa katika kisiwa cha Siu, kilicho karibu nakisiwa cha Pate, na eneo lililoko baina ya Pate na Faza.

Lahaja hii inakaribiana sana na lahaja ya kipate na kwa kiasi lahaja ya Kiamu.

Katika lahaja hii, sauti ‘ch’ hutumiwa pale ambapo katika Kiswahili sanifu pana sauti ‘t’.

Kwa mfano:

KISIU KISWAHILI SANIFU
dhiumbe viumbe
mbako baba yako
kufura kushiba
kuchuma kutuma
mchu mtu

KITIKUU/ KIBAJUNI

Ni lahaja inayozungumzwa kaskazini mwa Pate na Lamu kufikia Kismayu.

Mifano:

KITIKUU KISWAHILI SANIFU
nyawe Mama yako
kichoweo kitoweo
uwavu ubavu
nkuru mkubwa
peche pete

CHIMIINI/ CHIMBALAZI/ KIBARAWA

Hii ni lahaja inayotumiwa na wazungumzaji wa Kiswahili katika eneo la kati kati ya Mogadishu na Somalia.

Lahaja hii huzungumzwa katika maeneo ya Marka na Barawa, si ajabu baadhi ya wataalamu huizungumzia kama lahaja ya Kibarawa.

[email protected]

Marejeo

Massamba, D.P.B., (2002). Historia ya Kiswahili 50 BK. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Ipara, I. O., Waititu, F.G. (2006). Ijaribu na Uikarabati. Nairobi: Oxford University Press.

Habwe, J. (2006). Darubini ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers.

Maddo, U., Thiong’o, D. (2006). Mazoezi na Udurusu: Kiswahili 102/2. Nairobi: Global Publishers.

You can share this post!

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Lafudhi katika lugha ya Kiswahili

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Lahaja

adminleo