• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
Malkia Strikers yatumia wembe ulionyoa Rwanda na Ethiopia kukata Uganda na kuingia All-African Games 

Malkia Strikers yatumia wembe ulionyoa Rwanda na Ethiopia kukata Uganda na kuingia All-African Games 

Na GEOFFREY ANENE

KENYA ilitolewa kijasho na Uganda katika seti ya kwanza kabla ya kuwanyoa seti 3-0 katika mechi ya mwisho ya Ukanda wa Tano na kufuzu kushiriki voliboli ya wanawake kwenye mashindano ya Bara Afrika (All-African Games) Jumanne katika ukumbi wa Lugogo jijini Kampala.

Malkia Strikers ilikuwa alama moja tu mbele ya Uganda 21-20 katika seti ya kwanza kabla ya kushinda wenyeji hao 25-20.

Baada ya kubabaishwa katika seti ya kwanza, Kenya ilirejea katika seti mbili zilizofuata kwa nguvu zaidi na kuzinyakua 25-17, 25-16, mtawalia.

Majirani hawa waliingia fainali wakiwa wamechapa Rwanda na Ethiopia.

Kenya ilikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kufuzu kutetea ubingwa wake wa Afrika kwa sababu haikuwa imepoteza seti ikilinganishwa na Uganda iliyohitaji ushindi dhidi ya Wakenya kutokana na kuwa ilikuwa imekubali Rwanda kushinda seti moja.

‘Uganda mlima’

Baada ya mechi hii ambayo Jane Wacu, Mercy Moim, Edith Wisa, Triza Atuka, Noel Murambi, Violet Makuto na Agrippina Kundu walianzishwa, kambi ya Kenya iliyojawa na furaha ilikiri kwamba Uganda haikuwa timu rahisi.

“Kazi nzuri kutoka kwa kila mchezaji wetu. Tulitarajiwa kama mabingwa wa Afrika kuwa na presha. Hata kama tumeibuka na ushindi, bado kuna kazi kubwa ya kufanya ili tuwe imara,” Mwitaliano Shailene Shamdoo alisema.

Mkufunzi mkuu wa klabu ya KCB, Japheth Munala, ambaye pia ni mmoja wa makocha wa Malkia Strikers, alisema, “Ilikuwa mechi ngumu sana. Kweli, Waganda wameimarika sana. Kilichotusaidia sana kuwazima ni ‘service’ zetu na jinsi tulivyozuia makombora yao. Nafurahi sana kwamba tumefuzu kuenda nchini Morocco kutetea taji letu.”
Malkia Strikers inatarajiwa kurejea nchini kutoka Uganda hapo saa tisa kasorobo alasiri Jumatano. Mashindano ya All-African Games ni Agosti 19-30 mwaka 2019 nchini Morocco

You can share this post!

Waliouzia NYS bidhaa hawajalipwa miaka 4 baadaye

IEBC yatangaza upya nafasi ya Chiloba baada ya watu...

adminleo