• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:20 AM
Kundi lamtetea Oparanya kwa kuhudhuria hafla ya Jubilee

Kundi lamtetea Oparanya kwa kuhudhuria hafla ya Jubilee

Gavana wa Kakamega Bw Wycliffe Oparanya. Picha/ Maktaba

Na SHABAN MAKOKHA

KUNDI la wanasiasa kutoka Kaunti ya Kakamega, limemtetea Gavana Wycliffe Oparanya kutokana na hatua yake ya kuhudhuria sherehe ya kukaribishwa nyumbani ya waziri wa Michezo, Rashid Mohammed Echesa.

Wanasiasa hao walikuwa wakijibu madai yaliyotolewa na baadhi ya viongozi wa chama cha ODM, ambao walimshutumu Bw Oparanya kwenda katika sherehe hiyo, iliyohudhuriwa na Naibu Rais William Ruto.

Kundi la madiwani wa zamani kutoka maeneo ya Butere na Mumias walisema Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna anafaa kufahamu kuwa Bw Oparanya ni miongoni mwa vigogo wakuu wa chama hicho.

Wakiongozwa na Michael Keya, madiwani hao wa zamani walisema Bw Oparanya amewekeza rasilimali nyingi katika chama cha ODM hivyo hafai kudunishwa.

Bw Sifuna na wabunge Samuel Atandi (Alego Usonga) na Caleb Amisi (Saboti) walimshambulia Bw Oparanya huku wakimtaka kuhudumia wakazi wa Kakamega badala ya kujihusisha na siasa za urithi wa kisiasa kabla ya uchaguzi wa 2022.

Watatu hao walimtaka Bw Oparanya kushirikiana na kiongozi wa ODM Raila Odinga.

Bw Sammy Aina aliyewania kiti cha seneta wa Kakamega katika uchaguzi wa Agosti 8, mwaka jana lakini akapoteza, aliwataka wanasiasa wa NASA kukoma kumshambulia Gavana Oparanya kwa kuhudhuria sherehe za kumkaribisha Bw Echesa.

You can share this post!

‘Marehemu alifichua waliomuua kabla ya kufa’

Idara yatabiri kupungua kwa mvua kuanzia Jumatano

adminleo