• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
SHANGAZI AKUJIBU: Nilifumania mke nikamuacha, wa zamani ananitaka

SHANGAZI AKUJIBU: Nilifumania mke nikamuacha, wa zamani ananitaka

Na SHANGAZI SIZARINA

Hujambo shangazi? Nilikuwa nimeoa lakini nikamuacha mke wangu nilipomfumania na mwanaume mpango wake wa kando. Bado sijaoa tena na sasa mwanamke aliyekuwa mpenzi wangu anataka tuwe na uhusiano wa pembeni ingawa ameolewa. Ananiambia mume wake ni mtu wa shughuli nyingi na huwa anamuachia baridi sana. Bado ninampenda lakini sitaki kuvunja ndoa yake. Naomba ushauri wako.
Kupitia SMS

Ni muhimu kuheshimu ndoa ya mwanamume mwenzako hata kama mwanamke huyo alikuwa mpenzi wako. Ukweli ni kwamba mkishikana tena kisha mume wake ajue kutakuwa na shida. Ni heri utafute mwanammke ambaye hajaolewa.

 

Nimegundua ana mke baada ya miaka miwili
Salamu kwako shangazi. Nimekuwa na mwanaume mpenzi wangu kwa miaka miwili sasa na nimegundua majuzi tu kuwa ana mke. Jambo hilo limeniudhi sana kwani hajawahi kuniambia lakini nashindwa kumuacha kwa sababu nampenda kwa moyo wangu wote. Naomba ushauri wako.
Kupitia SMS

Umejua ukweli kwamba mwanaume huyo alikudanganya kwa kutokwambia kuwa ana mke. Na ingawa unasema unampenda sana, huwezi kubadili ukweli kwamba ana mke. Sasa ni juu yako kuamua iwapo utaendelea kuwa mpango wake wa kando ama utamuacha utafute mwingine.

 

Amedokeza anipenda
Shikamoo shangazi? Kuna kijana fulani ambaye amenidokezea kuwa ananipenda nami pia nampenda. Tatizo ni kuwa yeye amemaliza masomo ilhali mimi bado. Naomba ushauri wako.
Kupitia SMS

Ushauri wangu kwako ni kuwa huu si wakati unaofaa kwako kuanza mahusiano ya kimapenzi kwa sababu bado wewe ni mwanafunzi. Unahitaji kumakinika masomoni ili uweze kufaulu katika mtihani wa mwisho. Mwambie kijana huyo asubiri umalize shule.

 

Nawaona wanaume wote kama shetani
Nina umri wa miaka 24 na niliachana na mume wangu niliyempenda sana baada ya kunitendea unyama. Tangu wakati huo imekuwa vigumu kwangu kuwa na mapenzi ya dhati na mwanaume yeyote kwani kwangu kila mwanaume ni kama shetani. Bahati mbaya ni kwamba bado sijazaa na natamani sana kuwa na mtoto. Nifanye nini?
Kupitia SMS

Pole mwanangu kwa yaliyokupata ingawa hujaelezea kwa kina. Ni kweli kuna jambo unaloweza kutendwa na mtu umchukie yeye, jamaa zake na binadamu kwa jumla. Lakini nitakukosoa kuwa kitendo au vitendo vya watu fulani wabaya haviwezi kuwafanya watu wote kuwa wabaya. Dunia hii ina wabaya na wazuri pia. Usikate tamaa katika kutafuta mume mwingine kwani naona wewe bado ni mchanga. Kila la heri.

 

Namshuku rafiki
Hujambo shangazi. Ninashangaa kuhusu kinachoendelea kati ya mpenzi wangu na mwanaume rafiki yangu. Sote tunasoma chuo kikuu na siku za hivi majuzi nimewapata mara kadhaa wakipiga gumzo na kucheka. Nimemuuliza mpenzi wangu akasema hakuna chochote kati yao. Tafadhali nishauri.

Inawezekana uhusiano wao ni ule tu wa mwanafunzi kwa mwenzake. Huwezi kukata kauli kuwa wawili hao wana uhusianowa kimapenzi kwa kuwa umewapata wakizungumza. Iwapo unashuku kuna kitu kinachoendelea kati yao, chukua muda wa kutosha uchunguze ili ukweli.

 

Ananiudhi sana
Shikamoo shangazi. Kuna msichana ambaye nimemwambia wazi kuwa ninampenda lakini ananiudhi kwa kunipuuza. Nikimpigia simu ama kumtumia SMS hajibu. Tabia yake hiyo inaniumiza sana moyoni. Nifanye nini?
Kupitia SMS

Huyo bado si mpenzi wako kwa hivyo sielewi ni kwa nini unaumia moyoni akikosa kujibu simu zako. Hiyo ni kuonyesha kuwa hakujali na kwangu mimi naona unapoteza wakati wako ukimfuata.

 

Nimepata fununu ana mwingine
Vipi shangazi? Nina mpenzi ninayempanda kwa dhati. Hata hivyo nimesikia fununu kuwa ana uhusiano na mwanamke mwingine. Habari hizo zimenitia tumbo joto na sasa nafikiria kumuacha. Naomba ushauri wako.
Kupitia SMS

Si vyema kuchukua hatua kwa kutegemea uvumi kutoka kwa watu. Inawezekana kwamba watu wanaoeneza habari hizo ni maadui zake na nia yao ni kuvuruga uhusiano wenu. Itakuwa bora ukimuuliza mwenyewe.

 

You can share this post!

NYOTA YAKO: MACHI 07, 2018

Rais wa China akaangwa kwa nia yake ya kusalia madarakani...

adminleo