• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
Mashtaka ya uchochezi dhidi ya Kuria yafutwa

Mashtaka ya uchochezi dhidi ya Kuria yafutwa

Na RICHARD MUNGUTI

MKURUGENZI wa Mashtaka ya Umma (DPP) Jumatatu alitia kikomo ushahidi dhidi ya Mbunge wa Gatundu kusini Moses Kuria huku shahidi akikiri kortini hakuchunguza ipasavyo kanda ya video inayomnukuu mwanasiasa huyo akichochea umma dhidi ya kinara wa chama cha ODM Raila Odinga.

Katika kanda hiyo Bw Kuria amenukuliwa akitamka maneno ya uchochezi dhidi ya Bw Odinga huku akiwasihi wakazi wa Mlima Kenya wasikubali kumpigia kura kinara huyo wa upinzani.

Matamshi hayo katika video hiyo iliyodaiwa ilinukuliwa Septemba 5, 2017 katika eneo la Wagige kaunti ndogo ya Kikuyu yako katika lugha ya Gikuyu.

Mshtakiwa alimweleza hakimu anaelewa bayana lugha ya Gikuyu, Kiingereza na Kiswahili.

“Ninafanyakazi katika mamlaka ya mawasiliano nchini CAK lakini mimi ni afisa wa polisi katika kitengo cha uhalifu wa kimitandao,” alisema Insp Tiha na kuongeza, “Kanda hii inamnukuu Bw Kuria akitoa matamshi ya uchochezi na uhasama wa kijamii.”

Mtaalamu wa uhalifu wa kimitandao Inspekta Alexande Mathenge Tiha alimweleza hakimu mkuu Francis Andayi kuwa alitumiwa kanda hiyo na Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Jinai (DCI) mnamo Septemba 11, 2017.

“Nilitumiwa mkanda huo wa video na DCI kuuchunguza kwa lengo la kubaini matamshi ya uchochezi na uhasama wa kikabila dhidi ya Bw Odinga,” alisema Insp Tiha.

Video iliyochezwa mahakamani kama ushahidi dhidi ya Moses Kuria. Picha/ Richard Munguti

Insp Tiha alisema DCI alimtaka aukague mkanda huo kisha “atoe ushauri kuhusu matamashi ya uchochezi na uhasama aliodaiwa kautamka Bw Kuria na aliyekuwa Seneta wa Machakos Johnstone Muthama.”

Afisa huyo aliucheza mkanda huo mbele ya Bw Andayi na kutoa maelezo.

Akihojiwa na wakili Francis Munyororo Insp Tiha alisema “ripoti yake ni tofauti kabisa na shtaka linalomkabili Bw Kuria.”

Katika shtaka hilo inadaiwa Bw Kuria aliwataka wapiga kura 70,000 waliompigia Bw Odinga kura wasakwe.

“Je, katika ripoti uliyowasilisha hakuna mahala Bw Kuria amenukuliwa akitaka wapiga kura 70,000 waliompigia kura Bw Odinga wasakwe, ile ulitoa ripoti iliyotofauti?” Bw Munyororo alimwuliza afisa huyo wa polisi anayehudumu katika mamlaka ya mawasiliano CAK.

“Ni kweli ripoti yangu iko tofauti,” alijibu Insp Tiha.

“Ni ukweli ulienda kinyuma na matakwa ya DCI na ukatoa ripoti ambayo haikutakiwa na DCI kumuhusu Bw Kuria,” Bw Munyororo alimtaka Insp Tiha afafanue.

“Ni ukweli,” alijibu.

Akimjibu Bw Andayi afisa huyo wa polisi alikiri alitenda yale hakutakiwa na kutoa ushauri ambao haukutakiwa kumuhusu Bw Kuria.

Bw Kuria alieleza mahakama atakuwa akiiomba imwachilie kwa vile hakuna ushahidi unaomlenga katika kesi aliyoshtakiwa miaka miwili iliyopita. Amekanusha shtaka dhidi yake na yuko nje kwa dhamana.

Hakimu atapokea ushahidi wa Bw Kuria Juni 27, 2019.

 

You can share this post!

FKF yatangaza mipango ya Stars dhidi ya DR Congo

Dereva ndani miaka 15 kwa kumuua mpenziwe

adminleo