• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
JAMVI: Wabunge waonekana kutoelewa makubaliano ya Uhuru na Raila yanakoelekea

JAMVI: Wabunge waonekana kutoelewa makubaliano ya Uhuru na Raila yanakoelekea

Na CHARLES WASONGA

HUKU mwafaka kati ya Rais Uhuru Kenyatta na Kiongozi wa Upinzani Raila Odinga ukiendelea kuibua hisia mseto imebainika kuwa wabunge wa pande zote mbili hawaelewi mwelekeo utakaochukua.

Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa sasa wanaelezea hofu kwamba huenda hali hii ikalemaza juhudi za kuafikiwa kwa masuala muhimu yaliyoangaziwa katika taarifa ya pamoja iliyotiwa saini na viongozi hao.

Akiwasilisha hoja ya kuhimiza wabunge kukumbatia maelewano hayo Jumatano, kiongozi wa wachache katika bunge la kitaifa John Mbadi alisema wawili hao walikubaliana kuhusu masuala yenye umuhimu kwa maendeleo ya nchi.

Lakini akaeleza: “Sisi kama wafuasi wao tumekubali kuunga mkono mipango ya kuchochea maendeleo nchini. Kwa hivyo, tunasubiri mapendekezo hayo ili tuyajadili na kuyaelewa kabla ya kuyapitisha.

 

Mambo muhimu

Bw Mbadi, hata hivyo, alioorodhesha masuala amabayo yamekuwa yakiibuliwa na muungano wa upinzani, NASA, tangu 2017 kama vile, haki katika uchaguzi, uhuru wa idara ya mahakama, ukabila, ridhaa kwa wahasiriwa wa fujo za kisiasa, vita dhidi ya ufisadi na kupigwa jeki kwa ugatuzi, kama yatakayoangaziwa katika mazungumzo hayo.

Mwenzake upande wa Jubilee, Aden Duale naye alionekana mwenye ufahamu finyu kuhusu misingi na muundo wa mwafaka huo.

Kiongozi huyo wa wengi akasema: “Wakati huu muafaka huo ungali mchanga. Tungali kushuhudia mengi. Tumeonyeshwa ukurasa mmoja tu.”

Kiranja wa wachache Junet Mohammed ambaye aliandamana na Bw Odinga kwa mkutano na Rais Kenyatta katika jumba la Harambee, Nairobi Machi 9 pia hakutoa mwanga kuhusu yaliyojiri katika mkutano huo.

“Katika bungeni hili mimi niliyepewa nafasi ya kipekee ya kuandamana na kinara wetu katika mkutano huo. Nilisikiza yote na nikaridhika kabisa,” akasema bila kuelezea wenzake yale aliyoyasikia.

Bw Martin Andati sasa anasema kauli za wabunge hao, wandani wa karibu wa Rais Kenyatta na Bw Odinga, zinaonyesha wazi kuwa wao pia hawaelewi mambo mengi kuhusu muafaka huo.

“Hii ni kwa sababu ya maandalizi ya mkutano huo yalifanywa kwa siri kubwa, hali iliyopelekea vinara wengine wa NASA kulalamika walidai walifaa kuhusishwa,” anasema.

“Japo Wakenya wote wanakubali mkutano kati ya Raila na Uhuru ulipoesha joto la kisiasa nchini kufuata utata uliotokana na pande zote mbili zinafaa kutoa mwongozo utakaotumiwa kuendeleza mazungumzo kuhusu masuala yaliyoorodheshwa kwenye taarifa yao ya pamoja,” Bw Andati anasema.

 

Vioja bungeni

Ukosefu wa mwongozo mahususi kuhusu mwelekeo ambao ushirikiano kati Rais Kenyatta na Bw Odinga utachukua kutimiza malengo yao ndio ulichangia kioja kilichoshuhudiwa bungeni Jumanne alasiri.

Mbunge wa Mavoko Patrick Makau (Wiper) aliamua kuketi kwenye kiti kilichotengwa mahsusi kwa kiongozi wa wachache, Bw Mbadi. Alisema alichukua hatua hiyo baada ya kile alichodai kuwa “hatua ya ODM  kujiunga na Jubilee baada ya Raila kama kiongozi wake kuelewana na Rais Kenyatta.”

“Baada ya ODM kujiunga na Jubilee chama change cha Wiper ambacho ndicho cha tatu kwa ukubwa kimeniteua kuwa kiongozi wa wachache. Hii ndio maana niliketi katika kiti hicho,” aliwaambia wanahabari baada ya Spika Justin Muturi kumfurusha nje kwa kukaidi amri ya kumtaka ampishe Bw Mbadi.

Mwenzake wa Makueni Daniel Maanzo pia aliamua kukalia kiti cha Bw Junet (kiranja wa wachache) kwa sababu hiyo hiyo ya ODM kujiunga na Jubilee. Hata hivyo, aliondoka upesi kabla ya kuadhibiwa na Spika Muturi.

“Kwa sababu Raila, kama kiongozi wa ODM, hakuwahusisha wenzake; Kalonzo Musyoka (Wiper), Musalia Mudavadi (ANC) na Moses Wetang’ula (Ford Kenya) katika mkutano wake na kiongozi wa Jubilee, Rais Kenyatta, tunaamini kuwa amejiunga na Jubilee. Hii ndio maana niliketi katika kiti cha Junet na mwenzao Makau akaketi katika kiti cha Mbadi,” anaeleza Mbunge huyo ambaye ni wakili.

Bw Maanzo anasema Wiper itaunga mkono mazungumzo yatakayoendeshwa chini ya mpangilio “unaoeleweka na kuwekewa mihimili ya kesheria” na kujumuisha wadau wote.

 

‘Hakuna nusu mkate’

Ni  ufasiri aina hii uliomsukuma Bw Duale kufafanua kuwa mwafaka kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga haumaanishi kwamba kuna mipango ya kubuniwa kwa serikali ya mseto kati ya Jubilee na ODM.

“Hakuna nusu mkate hapa. Na chama cha ODM hakijamezwa na Jubilee kama inavyodaiwa. Sisi kama Jubilee tunataraji ODM kupiga msasa utendakazi wa serikali huku ikishirikiana nasi kusukuma ajenda ya maendeleo kwa manufaa ya Wakenya,” anasema.

Mbunge huyo wa Garissa Mjini anashauri vyama tanzu katika NASA kukoma kumkaripia Bw Odinga kwa kufuatua uamuzi wake wa kufanyakazi pamoja na Rais Kenyatta.

“Viongozi hawa wawili wameamua kuzika tofauti zao kwa ajili ya kuliunganisha taifa. Wiper, Ford Kenya na ANC ambao ni wenye hisa wadogo katika NASA wanapaswa kuheshimu uamuzi huu wa ODM,” anasema.

Kwa upande wake mchanganuzi wa masuala ya kisaisa Bw Odoyo Owidi anasema kukanganyikiwa huku kwa wanasiasa kunaweza tu kuondolewa ikiwa afisi kuu iliyobuniwa kushirikisha mazungumzo hayo itaanza kufanya kazi na kwa uwazi.

“Wakili Paul Mwangi na Balozi Martin Kimani walioteuliwa kuongoza afisi hiyo, kwa ushirikiano na washauri wengine, wanafaa kuanza kazi. Na watatekeleza majukumu yao kwa uwazi la sivyo hali hii ya wanasiasa kuendelea kurusha cheche za maneno huku na kule bado itaendelea,” anasema, akionya kuwa huenda hali hiyo ikavuruga malengo ya muafaka huu.

“Huu mkutano wa jumba la Harambee ulikuwa ni wa watu wawili. Sisi kama Wiper hauutambui wala kufahamu yaliyojadiliwa,” anasema.

Kauli yake inaungwa mkono na naibu kiongozi wa ANC Bw Ayub Savula ambaye anasema vyama tanzu ndani ya NASA viko tayari kuipa ODM “talaka” kwa kushirikiana na Jubilee.

You can share this post!

Kiyara aunda milioni kwa muda wa saa mbili Taiwan

JAMVI: Wimbi la ‘minjiminji’ layeyuka kama mvuke huku...

adminleo