• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
Rotich kung’olewa afisini baada ya kushtakiwa

Rotich kung’olewa afisini baada ya kushtakiwa

Na CHARLES WASONGA

WAZIRI wa Fedha Henry Rotich na maafisa wengine wa serikali ambao watafikishwa mahakamani Jumanne kwa tuhuma za kuhusika katika sakata ya wizi wa Sh21 bilioni za ujenzi wa mabwawa ya Arror na Kimwarer watasimamishwa kazi.

Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Noordin Haji Jumatatu alisema Rotich na wenzake sharti wajiondoe afisini baada ya kujibu mashtaka kadhaa yanayowakabili.

“Sharti waondoke afisini kwa muda… hawa sio magavana. Nitamwandikia Mkuu wa Utumishi wa Umma. Nitafanya hivyo sasa hizi. Hii ndio sheria.

“Ikiwa umeshtakiwa na ukajibu mashtaka, lazima ukae kando kwa muda kutoa nafasi kukamilishwa kwa kesi dhidi yako,” Bw Haji akawambia wanahabari alipoulizwa ikiwa itabidi washukiwa hao kuondoka afisini.

Jumatatu asubuhi Bw Haji aliamuru kukamatwa kwa Bw Rotich, Katibu wa Wizara ya Fedha Kamau Thugge na maafisa wengine 25 wa wizara hiyo na Halmashauri ya Ustawi wa Bonde la Kerio (KVDA) na NEMA kwa tuhuma za kuhusika katika sakata hiyo.

Maafisa hao watashtakiwa kwa makosa ya matumizi mabaya ya fedha, njama ya kutekeleza udanganyifu kinyume cha sheria, kuanza utekelezaji wa mradi bila kufanya maandalizi yanahitajika, kutozingatia sheria ya usimamizi wa fedha za umma na ukiukaji wa Sheria kuhusu utoaji wa zabuni kwa kuipa zabuni kampuni ya CMC di Ravenna kutoka Italia.

Kampuni hiyoilipewa zabuni ya ujenzi wa mabwawa ya Arror na Kimwarer katika kaunti ya Elgeyo Marakwet wenye thamani ya Sh63 bilioni.

You can share this post!

Korti yaambiwa Itumbi aliandika barua feki kuhusu mauaji ya...

Mtajutia kukubali serikali ya mseto, Ruto aonya

adminleo