• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 2:10 PM
Kisura ataka picha zake mtandaoni ili ajue polo anampenda

Kisura ataka picha zake mtandaoni ili ajue polo anampenda

Na LEAH MAKENA

KILELESHWA, NAIROBI

Mzozo mkali uliibuka kati ya wapenzi wa hapa pale kidosho alipojaribu kumlazimisha jamaa kuanika picha zake kwenye mtandao kama thibitisho kuwa alimpenda. Yasemekana jamaa alikutana na kipusa wiki moja baada ya kutengana na mpenzi wake wa awali.

“Kabla ya wawili hao kukutana, polo alikuwa na mchumba aliyekuwa amemtandaza kwenye mitandao yake yote ya kijamii,” alisema mdokezi.

Inasemekana jamaa alidinda kuziondoa picha hizo baada ya kutengana na mwanadada huyo akidai kuwa zilikuwa za kumbukumbu.

Licha ya kidosho kumsihi jamaa kuondoa picha hizo ili aweke zake, polo alisita na kusema kuwa mapenzi yake kwa mrembo yalikuwa rohoni na wala sio mtandaoni, jibu ambalo halikumridhisha kipusa.

Siku ya kioja, kidosho alikuwa amemtembelea  polo na alipopata simu yake, akavamia picha zilizokuwa kwenye mtandao na kuzifuta zote kwa matarajio kuwa jamaa angeweka zake.

Inasemekana kuwa polo alipandwa na mori kwa kitendo cha kidosho na hapo ndipo alimhakikishia kuwa kamwe hangetumia picha zingine kwenye mtandao.

“Mara ngapi nimekwambia sidhamini mapenzi ya mtandao? Unafaa kuelewa kuwa huwezi kunilazimisha kufanya jambo ambalo sitaki. Iwapo huna imani nami nimekupa uhuru wa kutafuta utakaowaamini,” polo aliteta.

Wadokezi wetu walisema kuwa, kidosho alitulia ila hatua ya kutoweka picha zake mtandaoni ilisalia kitendawili huku akishuku kuwa huenda polo alikuwa akiendeleza mazungumzo na mpenzi wake wa awali kwa lengo la kuzika tofauti zao na kurudiana.

Inasemekana demu ameanza kuchunguza mienendo ya jamaa kisiri kujua iwapo huwa anawasiliana na mpenzi wake wa zamani.

…WAZO BONZO…

You can share this post!

Mzee Moi arejea nchini baada ya matibabu Israeli

TAHARIRI: KEBS na ACA zimeshindwa kukabiliana na bidhaa...

adminleo