• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Gor kukabana na SuperSport United Confederations Cup

Gor kukabana na SuperSport United Confederations Cup

Na GEOFFREY ANENE

MABINGWA wa Kenya, Gor Mahia watapigania tiketi ya kuingia mechi za makundi za mashindano ya Afrika ya Confederations Cup dhidi ya SuperSport United.

Vijana wa kocha Dylan Kerr walikutanishwa na mabingwa hawa mara tatu wa Afrika Kusini katika droo iliyofanywa na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) Jumatano jioni jijini Cairo, Misri.

Gor ilijipata katika mashindano haya ya daraja ya pili baada ya kupigwa 1-0 na Esperance ya Tunisia mnamo Machi 18, 2018 na kubanduliwa nje kwa jumla ya bao 1-0.

Mechi ya mkondo wa kwanza kati ya Gor na Esperance ilimalizika 0-0 uwanjani Kenyatta mjini Machakos mnamo Machi 7.

Gor ilirejea nchini kutoka Tunis hapo Machi 19 asubuhi. Mabingwa hawa mara 16 wa Kenya wataalika SuperSport nchini Kenya mnamo Aprili 6 kabla ya kusakata mechi ya marudiano nchini Afrika Kusini hapo Aprili 17.

Klabu zingine kutoka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) zinazoshiriki Confederations Cup ni Rayon Sport (Rwanda), Al-Hilal Al-Ubayyid na Al-Hilal (Sudan) na Young Africans (Tanzania).

Rayon itakabiliana na Club Deportivo Do Sol kutoka Msumbiji nayo Yanga ichapane na Welayta Dicha kutoka Ethiopia katika mechi za kuingia makundi.

Al-Hilal Al-Ubayyid na Al-Hilal zitalimana na UD Songo (Msumbiji) na Akwa United (Nigeria), mtawalia.

Droo ya Klabu Bingwa Afrika pia imefanywa Jumatano. Kampala Capital City Authority (KCCA), ambayo ilipimana nguvu na Gor kabla ya kuanza kampeni yake, itapepetana na miamba Al Ahly (Misri) na Township Rollers (Botswana) na Esperance (Tunisia) katika Kundi A.

Kundi B linaleta pamoja TP Mazembe (DR Congo), Moulidia (Algeria), Difaa Hassani El Jadidi (Morocco) na E.S. Setif (Algeria).

Togo Port de Lome (Togo), Mamelodi Sundowns (Afrika Kusini), Wydad (Morocco) na Horoya (Guinea) ziko katika Kundi C nayo Zesco United, ambayo imeajiri Wakenya Jesse Were, Anthony Akumu na David Owino, iko Kundi D pamoja na Primeiro de Agosto (Angola), ESS (Tunisia) na Mbabane Swallows (Swaziland).

You can share this post!

Seneta Linturi apambana mahakamani kuhusu digrii

Ni kivumbi Kenya na Uzbekistan zikiumiza nyasi

adminleo