• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Kalonzo aandaliwa kuwarithi Uhuru na Raila

Kalonzo aandaliwa kuwarithi Uhuru na Raila

Na PIUS MAUNDU

BAADA ya mkondo wa kisiasa kuonekana kubadilika katika Muungano wa NASA, Wiper imeanzisha mikakati ya kuhakikisha kinara wake Kalonzo Musyoka amerithi ngome za kisiasa za Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga.

Mwenyekiti wa chama cha Wiper, ambaye ni Gavana wa Makueni, Prof Kivutha Kibwana sasa anasema kuwa Bw Musyoka, atahitaji baraka za Rais Uhuru Kenyatta na pia Raila Odinga kushinda urais 2022.

Mnamo Ijumaa, Prof Kibwana aliambia mkutano wa kamati za maendeleo kutoka vijijini kote kwa kaunti yake na viongozi waliochaguliwa katika eneo, kuwa hatua ya maridhiano iliyofanywa kisiri kati ya viongozi hao wawili, ndiyo itaamua siasa za 2022.

Ingawaje awali gavana huyo hakuwa amefurahishwa na hatua hiyo hasa kwa Bw Odinga kukosa kuwahusisha vinara wenza, alionya jamii ya Wakamba dhidi ya kumshtumu Bw Odinga ama kumhujumu Rais Kenyatta.

“Tunastahili kukosa kumshtumu Bw Odinga na badala yake tuanze kumuambia kuwa sisi ni sehemu ya salamu zile na Rais Kenyatta,” alieleza huku akiepuka kuhusu hatma ya muungano wa Nasa.

 

Mchezo safi

“Pia tunahitaji mabaraza za Rais Kenyatta,” alisema akiongeza, “Kuna njia tunaweza kupata baraka za Rais Kenyatta kwa kucheza vyema mchezo wetu kwa sasa.”

Wakati huo huo, akiongea kwa lugha ya Kikamba, Prof Kibwana alionya jamii hiyo dhidi ya kutojali jamii nyingine ambazo itazihitaji kwa Bw Musyoka kuweza kuingia Ikulu.

“Kuendelea mbele, lazima tujitahidi kuhusiana vyema na jamii zingine kwa sababu tutahitaji usaidizi wao kwa kijana wetu kuingia Ikulu,” alisema.

Pia aliunga mkono maoni ya Seneta wa Makueni Mutula Kilonzo Junior na mbunge wa Mbooni Erastus Kivasu, ambao wamekumbatia wazi maridhiano kati ya Bw Odinga na Rais Kenyatta na kusema yanafaa kutuliza na kuendeleza nchi.

Pia amekuwa akiwahimiza wenzake katika Wiper na Nasa kuangalia dhamira kubwa ya hatua hiyo na kuwacha manung’uniko.

“Hatutaki kiongozi wetu awachwe nje ya mkataba kati ya Bw Odinga na Rais Kenyatta tunapoelekea 2022,” Bw Kilonzo Junior aliambia mkutano katika kituo cha mafunzo ya Kilimo cha Kwa Kathoka, ambao ulihudhuriwa na viongozi waliochaguliwa.

Kulingana na Prof Kibwana, Wiper inashirikiana na vyama vingine vilivyowachwa nje ya mkataba wa awali na rais na wanalenga kufanya mkutano naye.

 

Tahadhari

Mbunge wa Kitui Kusini, Rachael Kaki na aliyekuwa Spika wa Bunge la Kaunti ya Makueni, Bw Stephen Ngelu wamemtahadharisha Bw Musyoka dhidi ya kuweka masharti akiwa anategea kuhusishwa kwa mkataba wa Bw Odinga na Rais.

Kuweza kusalia na umuhimu kisiasa, Bw Musyoka lazima akubali kufanya kazi na rais kwa sababu hatua ya hivi punde ya Bw Odinga imetia doa upinzani.

Bw Musyoka anatarajiwa kuongoza viongozi wote wa Ukambani kwa kongamano katika kaunti ya Machakos juma lijalo kujadili msimamo wa kisiasa wa eneo hilo kufuatia yaliyojiri.

Duru zimeambia Taifa Jumapili kuwa mojawapo ya ajenda kuu ni jinsi ya kumwandaa upya Bw Musyoka kumrithi Rais Kenyatta.

Bw Odinga amewaacha Wakenya wakiendelea kubahatisha kuhusu msimamo na mipango yake, hata ingawa tayari amezuru maeneo ya Kisii na Kisumu na kujaribu kufichua wazi mkataba baina yake na rais unahusu nini.

You can share this post!

Takwimu: Siaya yaongoza kwa idadi kubwa zaidi ya vifo nchini

Jirongo asimulia Raila alivyomsaidia kupata kazi Tanzania

adminleo