• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Kidume mkono gamu amhepa kisura wake dukani

Kidume mkono gamu amhepa kisura wake dukani

 Na TOBBIE WEKESA 

ROYSAMBU, NAIROBI

Mrembo mmoja alitamani ardhi ipasuke immeze kuepuka aibu aliyopata katika supamarket moja mtaani hapa baada ya polo aliyesemekana kuwa mpenzi wake kumhepa.

Kulingana na mdokezi, polo alikuwa amemtembelea mrembo anakoishi. Inadaiwa mrembo alimuomba polo amnunulie bidhaa fulani za matumizi  nyumbani.

Duru zinaarifu polo alimueleza mrembo waandamane naye supamaketi ili wakavinunue.

Ripoti zinasema mrembo alipofika supamaketi, aliamua kujaza troli na vitu visivyo na maana.

“Nilifikiri utachukua vitu unavyohitaji tu.  Sasa vibanzi, biskuti sharubati na popkons ni vya nini. Ama unapanga kununua supamaketi nzima,” polo alimuuliza mrembo. Badala ya kujibu swali, mrembo aliendelea kuongeza bidhaa kwenye troli.

Jamaa alilazimika kuanza kuondoa baadhi ya bidhaa kutoka kwenye troli.

Darling unajua tu si rahisi wewe kunifanyia shopping. Acha nijaze tu troli ndiposa vinisukume mwezi mzima,” mrembo alimueleza jamaa.

Duru zinasema jamaa aliamua kutoka nje ya supamaketi huku akimueleza demu asubiri akatoe  hela kwenye ATM.

Kipusa aliamua kumngoja polo hadi akachoka. Aliamua kumpigia simu lakini alikuwa mteja kwa muda mrefu na alipofaulu kumpata hakujibu.

Baada ya kugundua kuwa jamaa alikuwa amemhepa, alianza kuondoa bidhaa kwenye troli na kuvirudisha alikovitoa. Wahudumu wote kwa hiyo supamaketi walimrushia macho huku walinzi wakimakinika.

Kabla ya kumaliza kurudisha vitu, jamaa alimtumia  ujumbe kwenye simu akimuonya dhidi ya kutofuata maagizo yake.

“Wakati mwingine tukienda shopping, niulize kwanza nina pesa ngapi. Tabia yako ya kufanya mambo kwa kiburi ikome,” jamaa alimuonya mrembo kwa ujumbe.

Demu alilazimika kuondoka polepole bila kununua chochote.

…WAZO BONZO…

You can share this post!

TAHARIRI: Tuongeze juhudi kuangamiza TB

Mahakama yasitisha uchaguzi wa awamu ya pili Sierra Leone

adminleo