• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
PWANI: Wanawake waombwa kukubalia waume kuoa wake wengi

PWANI: Wanawake waombwa kukubalia waume kuoa wake wengi

Na MOHAMED AHMED

WANAWAKE wa Pwani wamehimizwa kuwakubalia waume zao kuoa wake zaidi ya mmoja ili kuwezesha kuongezeka kwa idadi ya watu eneo hilo.

Baraza la Maimamu na Wahubiri Nchini (CIPK) lilisema jana kuwa upanuzi wa ndoa ndio utakaowezesha idadi ya watu Pwani kuongezeka.

CIPK ilitoa pendekezo hilo kwa wanawake baada ya matokeo ya idadi ya watu yaliyotolewa Jumatatu kuonyesha kuwa kaunti tatu za Pwani zipo miongoni mwa zile zenye idadi ndogo zaidi ya watu.

Katibu mtendaji wa CIPK, Sheikh Mohammed Khalifa alisema pia kuna haja ya wakazi wa Pwani kuhimizwa kuoa wake zaidi.

“Tukiongeza ndoa ndipo tutapata watoto na kufanya idadi yetu kuwa ya juu zaidi. Tumekuwa tukiacha mafunzo ya dini na tamaduni zetu na kufuata mienendo ya wazungu kwa kuzaa watoto wachache,” akasema Sheikh Khalifa.

Alisema wanawake wakilegeza misimamo kwa waume wao kuhusu kuoa zaidi ya mke mmoja, na vijana nao watie juhudi za kuoa na kupata watoto basi idadi ya wakazi wa Pwani itaongezeka pakubwa.

Sheikh Khalifa alizungumza baada ya Taifa Leo kutoa kichwa cha habari katika gazeti lake la jana lililoeleza kuwa eneo la Pwani huenda likawa limelegea chumbani.

Kichwa hicho cha habari kilizua hisia tofauti nchini hususan kanda ya Pwani huku wakazi wa eneo hilo wakishinikiza wanaume kuwacha utumizi wa dawa za kulevya ambazo zinalemaza katika uzazi.

“Utumizi wa miraa na muguka umekuwa juu, jambo ambalo limechangia Wapwani kupata watoto wachache na ndiposa idadi yetu iko chini,” akasema Bw Khamis Omar, mkazi wa Mombasa.

Kulingana na takwimu za matokeo hayo, Kaunti ya Lamu ndiyo yenye watu wachache zaidi nchini kwa kuwa na watu 143,920 ikifuatwa na Isiolo ambayo ina watu 268,002.

Kaunti ya Samburu iliibuka na watu 310,327, huku Taita Taveta ikiwa na watu 340,671 nayo Tana River ikiwa na watu 315,943.

You can share this post!

Raila motoni kwa ‘kuwatusi’ mabinti Wakamba

SEKTA YA ELIMU: Undumakuwili huu wa TSC utakuja kuiponza...

adminleo