• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 2:16 PM
Raila amfokea Matiang’i kwa kudai majaji ni wakora

Raila amfokea Matiang’i kwa kudai majaji ni wakora

Na LEONARD ONYANGO

KINARA wa Upinzani Raila Odinga Jumatano amemkemea Waziri wa Usalama Fred Matiang’i kwa kudunisha Idara ya Mahakama.

Bw Odinga alisema matamshi yaliyotolewa na Dkt Matiang’i ambapo alitaja baadhi ya majaji katika Idara ya Mahakama kuwa ‘walaghai, wakora na waovu’, ni ya kiholela.

“Wiki nne zilizopita mimi na Rais Uhuru Kenyatta tuliafikiana kushirikiana katika kuleta amani ,” akasema Bw Odinga kupitia taarifa yake aliyotuma katika vyombo vya habari.

“Lakini nilikerwa mno kuona Waziri wa Usalama Fred Matiang’i akishambulia na kuwadhalilisha baadhi ya majaji wa mahakama kwa kutumia lugha ya kijeuri.  Matamshi hayo hayafai  kutolewa na afisa wa serikali,” akaongezea.

Bw Odinga alisema matamshi hayo ya Dkt Matiang’i ni sumu kwa mwafaka baina yake na Rais Kenyatta ambapo waliafikiana kuanzisha mchakato wa kuunganisha nchi mnamo Machi 9, 2018.

Bw Odinga aliwataka wabunge kukoma kutumia vikao vya kamati mbalimbali kuwa majukwaa ambapo maafisa wa serikali wanashambulia na kudunisha Idara ya Mahakama.

“Tumekuwa na kipindi kirefu cha sarakasi za kisiasa na sasa kila kiongozi ana jukumu la kuhakikisha kuwa tunakuwa na amani kwa kuepuka kutoa matamshi yanayogawanya nchi,” akasema Bw Odinga.

You can share this post!

Wabunge wataka kiini halisi cha kifo cha mwanafunzi wa...

Joho yu wapi? Kwa mwezi mzima ‘Sultan’ hasikiki

adminleo