• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Wahadhiri waagizwa kurejea kazini Jumatatu au wafutwe

Wahadhiri waagizwa kurejea kazini Jumatatu au wafutwe

Na OUMA WANZALA

WASIMAMIZI wa vyuo vikuu nchini wametishia kuwachukulia hatua kali wahadhiri ikiwa hawatarejea kazini kufikia Jumatatu Aprili 9.

Wakati wa mkutano na wanahabari jana katika Chuo Kikuu cha Kiufundi cha Nairobi (TUC), shirikisho la mabaraza ya vyuo vikuu (IPUCCF) liliwapa idhini wasimamizi wa vyuo vikuu kuwachukulia hatua wahadhiri watakaokosa kufika kazini Jumatatu.

“Hii ni kuwahimiza wasimamizi wa vyuo vikuu kuwachukulia hatua kali wahadhiri wa vyuo vyao ambao hawatafika kazini Jumatatu,” alisema mwenyekiti wa IPUCCF Profesa Paul Kanyari.

Aliwataka wahadhiri hao kutii agizo la Mahakama ya Leba na kurejea kazini na kuwaonya dhidi ya kuendelea kukaidi maagizo ya mahakama.
Kutokana na mgomo wa wahadhiri, vyama vingine vya wahudumu wa vyuo vikuu, KUSU na KUDHEIHA pia vimejiunga na mgomo huo.

Lakini wahadhiri wameapa kutorejea kazini ikiwa hawatatimizwa matakwa yao. Hii ni licha ya Mahakama ya Masuala ya Leba kuwataka kurejea kazini Jumatatu.

Kulingana na chama cha wahadhiri (UASU), tayari kimekata rufaa ya hukumu hiyo iliyotolewa Ijumaa.

Walisema mgomo utaendelea mpaka mahakama ya rufaa itoe uamuzi wake. Katibu Mkuu wa UASU Constantine Wasonga aliwataka wahadhiri kupuuza ilani zote zilizotolewa na wasimamizi wa vyuo vikuu.

Alisema mawasiliano yote yatatoka chamani humo mgomo unapoendelea na kuwataka kupuuza wasimamizi wa vyuo vikuu.

Ijumaa, Jaji wa Mahakama ya Masuala ya Leba Onesmus Makau alisema mgomo wa wahadhiri ulikuwa haramu na haukuwa umetambuliwa kisheria na kuwataka wahadhiri hao kurejea kazini. Jaji huyo alivitaka vyuo vikuu kuwasilisha mkataba wa makubaliano kati ya 2017 na 2021 kwa Waziri wa Leba katika muda wa siku 21.

Mahakama ya Rufaa inatarajiwa kutoa mwelekeo kuhusu hali hiyo Jumatatu. Mapema wiki hii, wahadhiri walifanya maandamano Nairobi na kuitaka serikali kuwasilisha ofa yake.

Migomo ya wahadhiri kuanzia mwaka jana imeathiri pakubwa mafunzo katika vyuo vikuu vya umma. “Vyuo vikuu vya umma havijaweza kupata nafuu kutokana na mgomo wa 2017 hali ambayo imeathiri masomo,” alisema Prof Kanyari.

Mgomo huo unaingia siku ya 40 Jumatatu.

You can share this post!

Mbunge akejeli wenzake kwa kumpigia debe Ruto

Msomi Mkenya apewa miezi 3 kuondoka Amerika

adminleo