• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Polo aandaa hafla ya kumtema mkewe

Polo aandaa hafla ya kumtema mkewe

Na TOBBIE WEKESA

WEBUYE MJINI

KALAMENI mmoja kutoka hapa alishangaza watu alipoandaa hafla ya kuachana na mkewe.

Inasemekana polo aliandikia marafiki na majirani barua ya mwaliko akiwaomba kuhudhuria hafla hiyo bila kukosa.

Kulingana na mdokezi wetu, kila mmoja aliyepokea mwaliko alipigwa na butwaa, kwani sababu aliyotoa polo ya kuachana na mkewe haikuwa na mashiko yoyote.

Mkewe alipogundua mpango wa kalameni, pia naye aliamua kuwaalika ndugu zake pamoja na marafiki kwa hafla hiyo.

Inadaiwa kipusa vile vile aliwadokezea wazee wa ukoo kuhusu njama ya mumewe.Siku ya hafla ilipowadia, kila mmoja aliyealikwa alihudhuria.

Polo alishangaa kuwaona mashemeji zake karamuni ilhali hakuwa amewaigta.Duru zinasema katika hafla hiyo, ni jamaa mwenyewe aliyekuwa mfawidhi.

“Mimi nimewaita hapa kuwajuza kwamba kuanzia kesho naanza maisha yangu upya. Nitakuwa kapera mchanga,” alisema wageni wakiangua vicheko.

Mkewe pamoja na ndugu zake walitulia tuli. Jamaa akaendelea: “Nimekaa na mke wangu kwa zaidi ya miaka kumi na wakati umefika wa kila mtu kurudi kwa mama yake. Uchumi umekuwa mbaya.”

Kabla polo kumaliza hotuba yake, wazee wa ukoo walifika. Hata hivyo, polo hakushtushwa na kuwasili kwao.

“Tumesikia mambo yako yote. Hebu tupe sababu nzuri ya kuachana na mkeo,” mzee mmoja alimuuliza mume huyo.

Kulingana na mdokezi, jibu la polo liliwaacha wengi vinywa wazi. “Miaka kumi kuishi na mtu mmoja kwa nyumba si rahisi. Aende kwao atafute bwana mwingine nami nitafute kidosho mwingine,” polo alidai.

Wazee walisitisha mkutano huo mara moja na kuwarai wote waliohudhuria kuachana na porojo za polo.

Kila mgeni aliondoka na kuelekea kwake huku wakistaajabishwa na kisanga cha jamaa huyo.

You can share this post!

DINI: Ukitaka kufanikiwa katika hatua zako maishani, lazima...

TAHARIRI: Malumbano haya yasiue ndoto ya BBI

adminleo