• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Walimu wanaochochea wanafunzi kugoma waonywa

Walimu wanaochochea wanafunzi kugoma waonywa

Na MUNEENI MUTHUSI

SUALA la baadhi ya walimu kuchochea migomo miongoni mwa wanafunzi shuleni liliangaziwa pakubwa hapo Jumatatu katika mchezo “Zahama” uliowasilishwa na shule ya upili wa wasichana ya Kichaka Simba kutoka kaunti ya Kwale.

Jumatatu ikiwa siku ya mwisho ya tamasha za michezo ya kuigiza kwa shule na vyuo ukumbini Lenana School, jijini Nairobi, mchezo huo uliibua uliibua hisia kali ukumbini.

Hayo yalikuwa wakati mchezo ulipofika hatua ya wanafunzi wa kidato cha tatu na cha nne walivyokula njama kuchukua mafuta ya petroli na kujaribu kuwachoma wenzao wa vidato vya kwanza na pili.

Ukumbi ulitulia tuli huku mioyo ya baadhi ya hadhira ikidunda dunda kana kwamba lilikuwa tukio la kweli lilivyokuwa likiendelea.

Wanafunzi hao walimwaga mafuta katika mabweni ya kidato cha kwanza na cha pili huku hadhira ikidundwa na roho, mmoja wa hao wanafunzi waasi alichukua kiberiti na kuwasha moto. Moto uliwaka kote mabwenini.

Lakini kwa bahati nzuri hayo mabweni hayakuwa na wanafunzi, kwani walikuwa wametahadharishwa na mmoja wa hao waasi (Karema) na kutorokea usalama kwengineko.

Swali ni, chuki hii dhidi ya wenzao waliitoa wapi? Walichochewa na mwalimu mwandamizi (Mwalimu Chocha) walipokataa kutekeleza njama yake ya kumkataa mwalimu mwenzake (mwalimu Tulivu).

Lakini ngoma ya kitamaduni kutoka St. Philips Mukomari ukanda wa Magharibi ilikuwepo kuziosha dukuduku zilizokuwa zimejijenga katika nyoyo za hadhira.

Katika densi hiyo kwa jina “Sonia” iliyopigwa kwa miondoko ya tamaduni ya Kiluhya, hatua kwa hatua ilionyesha kwa nini uwiano wa kifaifa ni muhimu kwa maisha yetu.

Wanafunzi walifanyikiwa kuonyesha hadhira kwamba baadhi ya matamshi ya chuki na kauli za kikabila zinazoendelezwa humu nchini, zinaweza kuwa na madhara makubwa, hata kwa wanaozitoa.

Vile vile shule ya upili ya wasichana ya Riara Springs, ambao ni wenyeji kutoka Jijini Nairobi walisisimua kupitia kwa mchezo wao “Scars of Yesterday”.

Mchezo huo ulitoa onyo dhidi ya tabia ya kutoyatambua na kujifunza kutokana na makosa ya siku za nyuma.

Mchezo huu hasa ulisisimua kwa vifaa ambavyo waigizaji hao walivitumia kuwasilisha ujumbe wao.

Baada ya kutamatika kwa mashindano hayo, sasa washindi kutoka kila kitengo watapata fursa ya kumtubuiza rais.

You can share this post!

Madaktari wa mitishamba wasifu marufuku ya ukataji miti

Buda afumania mkewe peupe akigawa asali sebuleni

adminleo