• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
DINI: Kipindi cha mfungo wa Kwaresma ni wakati wa kuonyesha ukarimu na huruma kwa wote

DINI: Kipindi cha mfungo wa Kwaresma ni wakati wa kuonyesha ukarimu na huruma kwa wote

Na FAUSTIN KAMUGISHA

WAKATOLIKI pote duniani wameanza mfungo wa Pasaka wa siku arobaini.

Kipindi hiki kinaitwa Kwaresima na kinafunguliwa rasmi kwa kupakwa majivu kwenye paji la uso.

Ni kipindi cha kufanya toba, kufunga, kusali na kutenda matendo ya huruma.

Siku arobaini zinaunganishwa na siku arobaini ambazo Bwana Yesu alishinda jangwani akifunga.

Tunasoma hivi katika Biblia, “Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi. Akafunga siku arobaini mchana na usiku.” (Mathayo 4: 1-2).

Bwana Yesu Kristo alikuwa anajiandaa kuanza kazi yake rasmi. Siku arobaini ni ishara ya kipindi cha majaribu, majaribio na taabu.

Siku arobaini ni kipindi cha maandalizi. Kujiandaa ni kujiandaa kushinda.

Namba arobaini inapatikana katika methali na misemo mbalimbali. Kuna msemo wa Waingereza kwamba, “Maisha yanaanza ukigonga miaka arobaini (Life begins at forty).”

Unapogonga miaka arobaini unakuwa umefikia kipindi cha mapumziko cha mchezo wa maisha.

Unatoka kwenye mafanikio unaingia awamu ya kuacha urithi.

“Kuwaelewa watu lazima kuishi nao siku arobaini” (Methali ya Waarabu).

Namba arobaini imetajwa mara 146 kwenye Biblia. Arobaini ni kipindi cha somo la unyenyekevu kwa wana wa Israeli. Waisraeli walizunguka miaka arobaini kabla ya kuingia nchi ya ahadi.

“Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana Mungu wako alikuongoza miaka arobaini katika jangwa, ili kukujaribu na kuyajua yaliyo moyoni mwako” (Kumbukumbu la Torati 8: 2).

Musa alikuwa mlimani Sinai siku arobaini. “Musa aliingia ndani ya wingu. Akaupanda mlima, akashinda huko siku arobaini mchana na usiku” (Kutoka 24:18).

Bwana Yesu alifunga siku arobaini. Tangia ufufuo wa Yesu na kupaa kwake mbinguni ni kipindi cha siku arobaini.

Kwaresima ni siku arobaini. Namba arobaini inapatikana kwa kuzidisha 5 mara 8. Tano ni ishara ya neema ya Mungu. Ikizidishwa kwa yenyewe ni neema juu ya neema (Yn 1:16).

Nane ni ishara ya mwanzo mpya. Kumaliza ni kuanza. Yesu alitahiriwa siku ya nane.

Arobaini ni kipindi cha muungano bora kati ya Mungu na watu wake kupitia kutoa.

“Je, mlinitolea sadaka na matoleo jangwani muda wa miaka arobaini, ee nyumba ya Israeli? (Amosi 5:25).

Kipindi cha siku arobaini ni kipindi cha ukarimu. Kufunga ni ukarimu. “Tunachoacha kwa kufunga kitolewe kama sadaka kwa maskini” (Papa Leo I).

Tuwe wakarimu kwa wasio wakarimu. “Tendo la ukarimu wa kiwango cha juu sana ni ukarimu kwa wasio wakarimu” (Joseph B. Buckminster).

Ukarimu unaona hitaji. “Hakuna barabara ya juu zaidi kuliko barabara ya ukarimu; ni wanyenyekevu tu hupitia barabara hiyo” (Mt. Augustino).

Kuna aliyemuuliza malaika, “Niendelee kutoa mpaka lini?” Malaika alimjibu, “Mpaka hapo Mungu atakapoacha kukupa.”

Kama ulishawahi kuwa mhitaji utafurahia utoaji. Kuwasaidia wale walio katika hali yoyote ya kuhitaji ndiko kunafanya mfungo uwe wa kumpendeza Mungu.

Arobaini ni mwarubaini. Mwarubaini ni mti mchungu wenye matawi yaliyotanda, maua na majani madogo. Huaminiwa katika utengenezaji wa dawa za maradhi mbalimbali.

Kanisa Katoliki husali kipindi cha siku arobaini. “Tunapofunga, unazuia vilema (udhaifu) vyetu, unainua mioyo yetu, unatujalia nguvu na tuzo; kwa njia ya Kristu Bwana wetu” (Utangulizi, Kwaresima IV).

Vilema saba vya dhambi ni: majivuno, uroho, uzinifu, hasira, ulafi, ulafi, kijicho na uzembe. Kufunga kunasaidia kudhibiti udhaifu huu.

Kwa msingi huo arobaini ni mwarubaini. Lengo la kufunga siku arobaini ni kumrudia Mungu.

“Mungu anapotoweka, lengo linatoweka. Lengo linapotoweka, maana inatoweka, thamani inatoweka, na maisha yanafia mikononi mwetu,” alisema Carl Jung.

Kumrudia Bwana kunahitaji nidhamu ya kufunga, kusali na kuwasaidia maskini.

You can share this post!

KINAYA: ‘Ouru’ hapaswi kuvuruga vita vya ‘Baba’ na...

Jombi aacha mke na kurudi kwao

adminleo