• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Watu 20 wafariki kwa kunywa pombe kuzuia kuambukizwa corona

Watu 20 wafariki kwa kunywa pombe kuzuia kuambukizwa corona

Na MASHIRIKA

WATU 20 wamefariki nchini Iran baada ya kunywa pombe yenye sumu kwa imani kuwa inaweza kuzuia kuambukizwa virusi vya corona.

“Baadhi ya wajinga wanafikiri unywaji pombe unazuia kuambukizwa virusi vya corona. Kutokana na imani hiyo watu 331 walikunywa pombe yenye sumu na 20 miongoni mwao wakafariki,” akasema msemaji mkuu wa wizara ya afya nchini Iran.

Wataalamu wa afya walisema ni imani potovu kuwa pombe ina kinga dhidi ya virusi vya corona. Wanashauri kuwa inaweza kutumika kuua viini kwa kunawa nayo mikono ama kuosha sakafu.

Hayo yalitokea Rais Marcelo Rebelo de Sousa wa Ureno akifungiwa nyumbani kwake kwa siku 14 kwa hofu huenda ameambukizwa virusi vya corona.

Hii imetokea wakati watu zaidi ya 110,000 walithibitishwa kuugua homa hiyo kote duniani kufikia jana, huku 3,882 kati yao wakifariki.

Mataifa yaliyoathiriwa zaidi ni China, Korea Kusini, Italia, Iran, Ufaransa na Ujerumani.

Kulingana na ofisi ya rais nchini Ureno, mnamo Jumamosi Rais Sousa alitangamana na wanafunzi na hata kupigwa picha nao, na baadaye mmoja wao akagunduliwa anaugua homa iliyozuka China mwishoni mwa mwaka jana.

Kufikia Jumapili kulikuwa na visa 30 vya homa hiyo nchini Ureno.

Nchini Marekani, Seneta Ted Cruz wa Texas pia amejifungia nyumbani kwake baada ya kufahamu alitangamana na kusalimiana kwa mkono na mtu ambaye alithibitishwa kuugua homa hiyo baadaye.

“Kama tahadhari nimeamua kujitenga nyumbani kwangu,” alisema Seneta Cruz mnamo Jumapili.

Homa hiyo pia ilimlazimu Papa Francis wa Kanisa Katoliki kukosa kufanya mahubiri ya Jumapili hadharani na badala yake akayapeperusha kupitia intaneti.

Ofisi ya Papa Francis ilisema hatua hiyo ililenga kuzuia watu kukusanyika katika ukumbi wa St. Peter’s Square kwa ibada ya Jumapili kama ilivyo kawaida, katika tahadhari dhidi ya virusi vya corona.

Haya yamejiri Italia ikitangaza marufuku ya kutoka ama kuingia mikoa miwili yenye visa vingi vya virusi vya corona.

Marufuku hiyo imeathiri watu milioni 16 katika maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo.

Kufikia jana Italia ilikuwa imethibitisha visa zaidi ya 7,000 vya maambukizi na vifo zaidi ya 350.

Waziri Mkuu wa Italia Giuseppe Conte aliweka sahihi marufuku hiyo Jumapili ambayo yataathiri maeneo ya Lombardy na Veneto ambako miji ya Milan na Venice inapatikana mtawalia.

Yeyote atakayekiuka marufuku hiyo anaweza kufungwa gerezani kwa miezi mitatu.

Shughuli za kawaida ambazo zimepigwa marufuku ni harusi, mazishi, mikahawa na shughuli zingine zinazokutanisha halaiki ya watu.

Kulingana na marufuku hiyo, mabaa yataendelea na shughuli lakini watu watatakiwa kukaa umbali wa futi tatu kutoka kwa mtu mwingine.

Wafungwa katika magereza manne waligoma kulalamikia marufuku hiyo hasa kuhusu kutembelewa na jamaa.

zao.

Ligi Kuu ya soka nchini Italia (Serie A) pia imetatizika baada ya serikali kuagiza mechi kuchezwa bila mashabiki.

Mnamo Jumapili mechi kati ya miamba wa Italia, Juventus na Inter Milan pamoja na nyingine kati ya AC Milan na Genoa zilichezwa bila mashabiki.

Mechi ya Ligi ya UEFA kati ya PSG ya Ufaransa na Borussia Dortmund ya Ujerumani nayo itachezwa kesho usiku bila mashabiki.

Wakati huo huo, maafisa wa afya nchini Zanzibar wamepiga marufuku watalii kutoka Italia kuzuru kisiwa hicho.

Waziri wa Afya Hamad Rashid alisema hatua hiyo inalenga kuzuia virusi hivyo kuingia nchini humo.

You can share this post!

Dawa ya kuzima Ruto kuingia Ikulu 2022 ni BBI – Atwoli

Msijaribu kuvuruga BBI Afraha, Tolgos aonya Tangatanga

adminleo