• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 8:55 AM
KAFYU: Polisi na majambazi sasa wazidisha uhalifu

KAFYU: Polisi na majambazi sasa wazidisha uhalifu

Na WAANDISHI WETU

VISA vya ukiukaji wa amri ya kutotoka nje usiku na uhalifu vimeendelea kushuhudiwa maeneo tofauti nchini huku maafisa wa polisi wakiwa mstari wa mbele kuvunja sheria wanayopaswa kutekeleza.

Mnamo Jumatatu usiku, maafisa saba wa polisi na raia wawili walikamatwa wakilewa katika baa moja mtaani Mbotela, Nairobi.

Maafisa hao wanahudumu katika makao makuu ya kitengo cha kukabiliana na uhalifu nchini.

Maafisa hao wanazuiliwa katika seli wakisubiri kufunguliwa mashtaka ya kukiuka kafyu ya serikali na kulewa baada ya muda unaoruhusiwa.

Usiku huo, watu watatu walikamatwa katika msako wa polisi kwa kufungua baa katika mitaa ya Lunga Lunga na Mukuru Kayaba, Kaunti ya Nairobi.

Polisi walitwaa mashine kadhaa za kuchezea kamari wakati wa kisa hicho.

Kamanda wa polisi katika eneo la Makadara, Bw Abdikadir Sheikh aliambia Taifa Leo kwamba lengo la msako huo lilikuwa kukabiliana na wanaokusanyika pamoja wakati huu wa janga la virusy vya corona.

“Baa ni moja ya mahali ambapo wananchi hukutania kuburudika pamoja. Serikali imeamuru watu kujiepusha kukaribiana ili ugonjwa wa corona usieneee zaidi, ” Bw Sheikh akasema.

Katika eneo la Nyakoe, Kaunti ya Kisii, polisi wanawasaka washukiwa waliomuua afisa mmoja wa Nyumba Kumi, aliyekuwa akitekeleza agizo la serikali la kuhakikisha maeneo ya burudani yanafungwa kulingana na amri ya serikali.

Afisa huyo aliuawa Jumatatu usiku katika baa moja inayopatikana Mosocho, eneobunge la Kitutu Chache Kusini. Afisa huyo aliyetambulika kama Japheth Mayieka, alikutana na kifo baada ya yeye na wenzake wawili kuingia katika baa hiyo inayodaiwa kutofuata maagizo yaliyowekwa na serikali

Inaaminika kuwa baa hiyo imekuwa ikihudumu usiku kucha na huwafungia walevi ndani.

Wakazi wa sehemu hiyo wamewataka machifu kukoma kutumia vijana kutekeleza maagizo ya serikali.

Kwingineko, katika sehemu za Nyatieko, hatua chache kutoka Nyakoe, wakazi wamelalamika kuwa kuna baa ya mtu maarufu inayohudumu hata baada ya muda ulioruhusiwa.

Katika tukio lingine la Malindi, Kaunti ya Kilifi, wakazi wa eneo la Migingo wanalalamikia kelele kutoka kwa walevi na wametaka hatua za sheria kuchukuliwa dhidi ya wanaofungua vilabu vya pombe usiku.

Akizungumza jan mjini Malindi, mkazi Kalume Chengo, alisema kelele hizo zinawakosesha usingizi wanaoishi karibu na vilabu na kuhatarisha usalama wao.

Kulingana na Bw Chengo, huenda hali hiyo ikawa changamoto dhidi ya vita vya kukabiliana na virusi vya corona na kuweka maisha ya wananchi kwenye hatari.

Wakati huo huo, Bw Chengo ameitaka idara ya polisi kuingilia kati na kuanzisha msako sehemu hiyo na kuwakamata wanaovunja sheria ya kutotoka nje usiku.

“Ninataka polisi waje hapa Migingo kwa sababu tabia hii inatunyima amani, hatulali na hatuwezi kuvumilia wakati tunapozidi kuumia,” alisisitiza Bw Chengo.

Kilifi ni moja ya kaunti nne ambazo wakazi wamepigwa marufuku kusafiri hadi katika kaunti nyingine kwa siku 21 kutokana na idadi kubwa ya watu walioambukizwa virusi vya corona.

Ripoti za Sammy Kimatu, Benson Matheka, Wycliffe Nyaberi na Alex Amani

You can share this post!

Marufuku yafuta kazi maelfu ya wananchi

Wazee wamlaani gavana kuzuia mbunge kuwapa chakula

adminleo