• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Ole Sapit aitaka serikali isambaze PPE kwa hospitali zinazosimamiwa na makanisa

Ole Sapit aitaka serikali isambaze PPE kwa hospitali zinazosimamiwa na makanisa

Na CHARLES WASONGA

KIONGOZI wa Kanisa la Anglikana Nchini (ACK) Askofu Mkuu Jackson Ole Sapit ametoa wito kwa serikali kusambaza vifaa vya kujikinga (PPE) katika hospitali zinazosimamiwa na makanisa wakati huu wa janga la Covid-19.

Alisema hatua kama hiyo itahakikisha wahudumu wa afya katika hospitali hizo pia wanakingwa dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona wanapowahudumia wagonjwa.

“Vifaa vya kujikinga vinavyotolewa kwa serikali na wahisani au kununuliwa kwa fedha zinazokusanywa visambazwe kote nchini katika hospitali za umma na zinazosimamiwa na makanisa,” Ole Sapit akasema wakati wa ibada ya Jumapili katika Kanisa la All Saints Cathedral, Nairobi.

Ibada hiyo ilipeperushwa kupitia runinga na mitandao kwani serikali imepiga marufuku ibada za kawaida kama sehemu ya mikakati ya kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.

Askofu Ole Sapit pia aliitaka serikali kusambaza pesa zinazotolewa na wahisani kama msaada wa kufadhili vita dhidi ya janga hilo kwa hospitali hizo ambazo zinakabiliwa na changamoto ya uhaba wa pesa wakati huu ambapo watu wengi hawaendi huko kwa matibabu.

“Unyanyapaa unaohusishwa na ugonjwa wa Covid-19 umechangia watu wengi kuogopa kwenda hospitalini. Hali hii imesababisha hospitali za makanisa kukosa fedha za kuwalipa wahudumu wao,” akasema.

Askofu Ole Sapit aliitaka serikali kuondoa ushuru unaotozwa vifaa vya PPE ili bei yavyo ishuke wakati huu ambapo vinahitajika kwa wingi.

You can share this post!

COVID-19: Kenya sasa ina visa 887

UEFA: Mipango ipo kukamilisha Champions League na Europa...

adminleo