• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
Ruto na Ichung’wa wakana kuwapa wakazi wa Kiambu chakula hatari

Ruto na Ichung’wa wakana kuwapa wakazi wa Kiambu chakula hatari

NA SIMON CIURI

Utata umeibuka kuhusu aliyetoa chakula cha msaada kilichopewa wakazi wa kaunti ya Kiambu Jumatatu ikidaiwa chakula hicho ni hatari kwa afya ya binadamu baada ya waliokipokea kulazimika kukirudisha.

Gavana wa Kiambu James Nyoro alisema kwamba watu 12 waliokula chakula hicho walikimbizwa katika hospitali za Tigoni, Kiambu na Thika baada ya kubebwa kutoka kwa nyumba zao kwa ambulansi.

Naibu Mshirikishi wa Kaunti ya Kiambu Wilson Wanyanga alisema kuwa chakula hicho kilipeanwa na mbunge wa Kikuyu Kimani Ichung’wa na kundi lililosemekana kuhusishwa na Naibu Rais William Ruto.

Lakini Dkt Ruto na Bw Ichung’wa walikana madai kwamba walihusika katika kupeanwa kwa chakula hicho kibaya huku ikiibuka kuwa kumekuwa na wahisani tofauti wa misaada ya chakula katika kaunti hiyo hivi karibuni.

Mkazi wa eneo la Gikambura David Githinji aliyepokea chakula hicho Jumapili alasiri aliambia Taifa Leo kuwa gari aina ya Land Cruiser ilifika mtaani humo na mtu aliyekuwa ndani yake akaita watu waje wapewe chakula na baadaye akaondoka.

“Ilikuwa ni mafuta ya kupikia, unga wa ugali na sukari. Tuligundua kwamba majani chai yalikuwa na rangi tofauti na ilikuwa chachu tulipoyatumia. Baadaye mmoja wa familia yangu akaanza kuwa na maumivu ya tumbo. Tumeandikisha taarifa hiyo kwenye kituo cha polisi,” Bw Githinji aliambia Taifa Leo.

Maafisa wa afya wa Kiambu walisema wamepeleka sampuli za chakula hicho kwa maabara kwa uchunguzi wa kisayansi kubaina iwapo kilikuwa na sumu.

Tafsiri: Faustine Ngila

You can share this post!

Covid-19: Visa vingine 72 vyaripotiwa

Wanawake wanne waacha watoto wao katika hospitali Thika

adminleo