• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
Uwezekano wa Serie A kurejelewa Juni 13 kujulikana Alhamisi

Uwezekano wa Serie A kurejelewa Juni 13 kujulikana Alhamisi

Na CHRIS ADUNGO

SERIKALI ya Italia itaamua mnamo Alhamisi Mei 28, 2020 iwapo wakati mwafaka wa kurejelewa kwa soka ya Ligi Kuu ya taifa hilo (Serie A) msimu huu umewadia au la.

Vikosi vinavyonogesha kivumbi cha Serie A vilikubaliwa kurejea mazoezi ya makundi ya watu 10 mnamo Mei 19 huku klabu zote 20 za ligi hiyo zikiafikiana kuanza upya kampeni za msimu huu mnamo Juni 13, 2020. Soka ya Italia ilisitishwa mnamo Machi 2020 kutokana na janga la virusi vya homa kali ya corona.

Wakati uo huo, Shirikisho la Soka la Italia (FIGC) limeteua Agosti 20, 2020 kuwa siku ya mwisho ambapo kampeni za Serie A zinastahili kuwa zimetamatika rasmi iwapo zitarejelewa Juni 13. Hii ni kwa sababu kampeni za msimu ujao wa 2020-21 zimeratibiwa kuanza rasmi mnamo Septemba 1, 2020.

Hadi kipute cha Serie A kilipoahirishwa, klabu za ligi hiyo zilikuwa zimesalia na mechi 12 kila moja muhula huu. Mabingwa watetezi Juventus wanaofukuzia ufalme wa taji la Serie A kwa mara ya tisa mfululizo msimu huu, wanaselelea kileleni mwa jedwali kwa alama 63, moja zaidi kuliko Lazio ambao ni wa pili.

Kwa mujibu wa FIGC, iwapo ligi yoyote kati ya tatu za madaraja ya juu nchini Italia itasitishwa pindi baada ya kurejelewa, basi washindi wa kila ligi na wale watakaoshushwa ngazi mwishoni mwa muhula huu wataamuliwa kwa njia ya mchujo.

Iwapo itakuwa vigumu kwa ligi hizo kukamilika kupitia mchujo, basi washindi wataamuliwa kwa matokeo yatakayokuwa yamesajiliwa na kila kikosi hadi kufikia wakati wa kusimamishwa tena kwa kampeni za muhula huu.

Ligi ya Daraja la Pili (Serie C) ndiyo inayowaumiza vichwa zaidi vinara wa FIGC hasa ikizingatiwa kwamba kipute hicho kinachojumuisha jumla ya klabu 60 tofauti ambazo zimegawanywa katika makundi matatu, kinakabiliwa na panda-shuka tele za kifedha.

You can share this post!

Huenda mzozo wa karo shuleni Makini ukatatuliwa kortini

Ukosefu wa ukaguzi wa kina mpakani Busia waibua hofu

adminleo