Habari

Ruto aendeleza juhudi za kuvutia vijana akitafuta Tutam

Na NDUBI MOTURI July 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto ameongeza juhudi za kuwavutia vijana kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 baada ya kuzindua mpango wa Sh2 bilioni wa kuwawezesha kupata ajira kupitia mafunzo kazini, nafasi za kazi za kidijitali na ushirikiano na sekta ya kibinafsi.

Mpango huo wa NextGen Youth Empowerment Programme, unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya serikali, Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) na sekta ya kibinafsi, unalenga kuwapa vijana ujuzi na uzoefu unaohitajika katika soko la ajira.

Hatua hiyo inajiri huku serikali ya Kenya Kwanza ikijaribu kurejesha imani ya vijana baada ya miezi kadhaa ya malalamiko kuhusu ukosefu wa ajira, ushuru mkubwa na gharama ya juu ya maisha.

Kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), zaidi ya Wakenya milioni 22.1 walikuwa wamejisajili kupiga kura mwaka 2022, huku walio na umri wa kati ya miaka 18 na 34 wakiwa zaidi ya nusu ya wapigakura wote.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo, Rais Ruto alisema serikali imeamua kuwekeza katika mipango inayounganisha elimu na ajira.

“Mafunzo kazini si kazi za muda tu. Ni daraja kati ya kujifunza na kujipatia kipato, kati ya uwezo na utendaji, na kati ya ndoto na mafanikio. Leo tunajenga daraja hilo kwa vijana wa Kenya kupitia mpango wa NextGen,” alisema.

Rais alikiri kuwa wahitimu wengi hukumbwa na changamoto ya kupata ajira kwa sababu waajiri wanahitaji uzoefu wa kazi kuliko vyeti vya kitaaluma.

“Waajiri wanatafuta uzoefu wa vitendo, nidhamu kazini na ujuzi unaohitajika na sekta mbalimbali. Vipaji vinapokosa nafasi, ndoto huchelewa kutimia na taifa hupoteza uwezo wake wa uzalishaji,” alisema.

Alisema vijana 100,000 walioajiriwa kama walimu chini ya serikali yake walipitia mafunzo kazini kabla ya kuajiriwa rasmi.

Aidha, wahitimu 5,600 wanapata mafunzo chini ya Mpango wa Makazi Nafuu, huku zaidi ya mafundi 2,000 wakipata vyeti kupitia mpango wa kutambua ujuzi.

Rais pia alisema zaidi ya vijana 1.9 milioni wamefunzwa ujuzi wa kidijitali, hatua iliyochangia kuundwa kwa nafasi za kazi 350,000 katika sekta hiyo.
Aliongeza kuwa zaidi ya Wakenya 580,000 kwa sasa wanafanya kazi nje ya nchi kupitia mpango wa serikali wa ajira majuu.