• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Wawili wanusuruka kifo katika ajali Thika Superhighway

Wawili wanusuruka kifo katika ajali Thika Superhighway

Na SAMMY WAWERU

WATU wawili Jumamosi wamenusurika kifo baada ya lori walimokuwa kuhusika katika ajali mbaya katika barabara ya Thika Superhighway eneo la Carwash, Githurai.

Wawili hao ni dereva wa lori la masafa marefu na kondakta wake.

Kulingana na dereva, lori hilo lenye nambari za usajili KBU 591R lilipoteza mwelekeo baada ya usukani wake kujiloki likiwa kwenye kasi.

“Ni kwa neema ya Mungu tumenusurika na halikuhusisha gari jingine,” akasema.

Usukani wa lori kujiloki na kutajwa kama tukio hatari barabarani linaloweza kusababisha maafa, kichwa cha lori hilo lililokuwa katika leni ya kasi, kilijipinda upande wa kulia na kung’oa vyuma kadhaa vya reli.

Lori hilo lililokuwa likielekea Nairobi hata hivyo halikuwa na mizigo.

Akithibitisha kisa hicho, afisa Antony Guchu wa kitengo tamba cha trafiki Thika Road, amehimiza madereva kuwa waangalifu na kuhakikisha magari yao yanakaguliwa iwapo yana hitilafu yoyote kabla kuingia barabarani.

“Kuendesha gari kwa mwendo wa kasi kunaua, mbali na kujihatarishia maisha yako mwenyewe kama dereva pia unahatarishia maisha ya watumizi wengine wa barabarani,” Bw Guchu akaonya.

Afisa huyo pia alihimiza madereva kuwa waangalifu hasa wanapobadilisha leni, ubadilishaji leni kiholela Thika Super Highway na uendeshaji gari kwa mwendo wa kasi ukilaumiwa kuwa kiini kikuu cha ajali nyingi.

Ajali hiyo imetokea siku kadhaa baada ya mwanamuziki Jimmy Walter Githinji maarufu kama ‘Jimmy Wayuni’ (Wa nyimbo za Benga kwa lugha ya Agikuyu) kupoteza maisha baada ya gari lake kuhusika katika ajali mbaya Thika Road, karibu na Chuo Kikuu cha Kenyatta, KU.

Ajali hiyo ya mnamo Jumanne usiku, inadaiwa gari la Wayuni liligongana na lori la kusafirisha mizigo, katika leni ya kasi.

You can share this post!

Lipeni karo hata kama shule zimefungwa – Serikali

Mwanatenisi Roger Federer sasa ndiye mwanamichezo...

adminleo