• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 2:10 PM
Chifu ajengewa ofisi mpya Ngoliba

Chifu ajengewa ofisi mpya Ngoliba

Na LAWRENCE ONGARO

WAKAZI wa Ngoliba, Thika Mashariki sasa wanaweza kupata huduma za chifu wao katika ofisi mpya.

Kabla ya kujengwa kwa hii mpya, walikuwa wanapata huduma zao kwenye ofisi ya matope kukiwa na changamoto tele.

Mbunge wa Thika Bw Patrick ‘Jungle’ Wainaina, alisema kwa zaidi ya miaka 15 hakuna ukarabati wowote uliofanyika katika ofisi hizo za awali.

“Ofisi hiyo imegharimu Sh1.5 milioni na imejengwa kisasa kupitia fedha za mgao wa serikali wa ustawi wa maeneobunge NG-CDF,” alisema Bw Wainaina.

Alisema kutokana na janga la corona linaloendelea kutikisa ulimwengu, machifu mashinani wana jukumu la kuwahamasisha wananchi.

Chifu wa eneo hilo Bi Alice Njoki Kago, alisema ofisi hiyo mpya tayari imeleta mwamko mpya sehemu ya Ngoliba na vitongoji vyake.

“Hapo awali kulikuwa na idadi chache ya watu waliofika ofisini kuleta malalamiko. Lakini tangu ofisi hii mpya ifunguliwe, watu ni wengi wanaofika hapa kuwasilisha malalamishi,” alisema Bi Kago.

Alisema wakati huu wa janga la corona wamechukua jukumu kuona ya kwamba wananchi wanahamasishwa kunawa mikono, kuvalia barakoa, na kujiepusha na mikusanyiko.

Muhimu zaidi aliwashauri wakazi wawe makini na wana wao hasa wakati huu ambapo wako nyumbani kwa likizo ndefu kutokana na janga la maradhi.

Alisema huu pia ni wakati wa wazazi kuwapa watoto wao majukumu mengine muhimu ya kijamii kama kufua nguo, kupika chakula, kuandaa nyumba, na pia kuwahamasisha kuhusu maisha yao ya baadaye.

Alisema wao – machifu – ndio jicho la serikali na watazidi kuchukua jukumu hilo la kuhamasisha wananchi kuhusu corona.

You can share this post!

COVID-19: Mashabiki wa Gor Mahia tawi la Nakuru watoa...

Jadon Sancho acheka na nyavu mara tatu kuiongoza Dortmund...

adminleo