• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Mzozo Knut wachacha huku Sossion akitupwa nje

Mzozo Knut wachacha huku Sossion akitupwa nje

Na BERNARDINE MUTANU

MZOZO katika Chama cha kitaifa cha Walimu (KNUT) uliendelea kutokota zaidi jana baada ya wanachama wa Kamati Kuu Simamizi (NEC) kutwaa afisi ya Katibu Mkuu Wilson Sossion na kumpa Hesbon Otieno.

Maafisa wa NEC Jumamosi walisema wanapanga kumuapisha Bw Otieno, kwa kuwa hawamtambui Bw Sossion.

Walitangaza hayo licha ya Bw Sossion kusisitiza kuwa ndiye Katibu Mkuu wa chama hicho baada ya kuenda mahakamani kuzuia kuondolewa kwake afisini.
Kamati hiyo jana ilitangaza kuwa tayari kuna mabadiliko ya uongozi ndani ya chama hicho.

Wakati wa mkutano na wanahabari jana katika afisi kuu za KNUT, Nairobi, wanachama wa NEC waliofika katika mkutano huo walisema tayari msajili wa uhusiano wa leba amethibitisha kupokea notisi ya mageuzi katika uongozi wa chama hicho.

“Kusimamishwa kazi kwa aliyekuwa katibu mkuu ndugu Sossion ni kuambatana na sheria. Tulituma ombi la mageuzi katika uongozi wa KNUT kuambatana na sheria ya uhusiano wa leba,” alisema Bw John Gitari Munyi, ambaye ni mdhamini katika bodi ya KNUT.

Alisema waliwasilisha ombi hilo Aprili 30 na kutoka wakati wa kuwasilishwa kwake kuendelea, Hesbon Otieno Agolla ndiye Kaimu Katibu Mkuu mpya wa KNUT.

Mnamo Alhamisi, msajili wa vyama vya leba Bw E. N Gicheha alithibitisha kusajili notisi ya mabadiliko yaliyoombwa bodi ya KNUT kumwondoa Bw Sossion kama katibu mkuu.

“Msajili ameeleza bayana kwamba kuna mabadiliko katika usimamizi wa KNUT. Kama wadhamini, tunajua kuna agizo la mahakama lakini agizo hilo lilitolewa baada ya msajili kuthibitisha mabadiliko ndani ya chama,” alisema Bw Gitari.

Wanachama hao hata hivyo walisisitiza kuwa hawakumwondoa Bw Sossion kwa sababu alikuwa amechaguliwa mbunge lakini kwa sababu ya kutowajibika kazini, udanganyifu na kuzembea kazini kuambatana na Kifungu cha 9 kipengee cha C7 cha katiba ya KNUT.

Walipuuzilia mbali tangazo la Bw Sossion kwamba ataitisha Kikao Maalum cha Wajumbe mwakani kwa kusisitiza kuwa ni NEC ndiyo yenye uwezo wa kufanya hivyo.

Viongozi hao kutoka maeneo mbali mbali nchini waliimba nyimbo za kumkashifu mbunge huyo maalum, na kumtaka kulenga siasa na kuachana na masuala ya walimu.

 

You can share this post!

Kaunti za Meru na Embu zapigania miraa

Madaktari watoa sindano 7 kutoka tumbo la mtoto

adminleo