• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 3:34 PM
Kipa Oluoch aikosesha Gor ushindi ugenini Rwanda

Kipa Oluoch aikosesha Gor ushindi ugenini Rwanda

Na JOHN ASHIHUNDU

Mashabiki wa Gor Mahia kwa mara nyingine wamefedheheshwa na uchezaji wa kipa Boniface Oluoch ambaye kosa lake liliisaidia Rayon Sports kufunga bao la kusawazisha katika sare yao ya 1-1, ugenini mjini Kigali.

Gor Mahia walitangulia kufunga bao katika mechi hiyo iliyochezewa Nyamirambo Stadium, Jumapili usiku.

Wakati huo huo, haijajulikana itakapochezewa mechi ya pili ya Mei 16 kati ya mabingwa hao wa ligi kuu nchini na klabu ya USM Alger ya Algeria, wakati huu maafisa wao wanasubiri kufahamishwa iwapo uwanja wa MISC Kasarani utakuwa umekamilika.

Akizungmza na waandishi jana, Naibu Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Ronald Ngala alisema jana kwamba huenda mechi hiyo ikaamishiwa Kenyatta Stadium mjini Machakos ikiwa uwanja wa Kasarani utakuwa haijakamilika.

“Tunangojea kufahamishwa kuhusu uwanja wa Kasarani ili tuwasiliane na CAF. Uwanja wa Machakos utabakia kuwa mbadala kwa sasa,” alisema.

USM Alger wanaongoza Kundi D baada ya kuitandika Young Africans ya Tanzania kwa 3-0 mwishoni mwa wiki, ambapo mechi yao dhidi ya K’Ogalo Jumatano ijayo ni muhimu kwa timu zote.

Sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Rayon Sport imewaacha Gor Mahia katika nafasi ya pili kwenye kundi hilo ambapo lazima waandishe ushindi katika mechi ijayo ili kufufua matumaini ya kusonga mbele ili kufuzu kwa hatua ya 16 bora.

Dhidi ya Rayon Sports, kipa wao chaguo la kwanza Boniface Oluoch amelaumiwa kutokana na bao walilofungwa dakika ya 24 kufuatia fri kiki ya Erick Rutanda in the 24thminute.

Oluoch, amewahi kufungwa mabao kama hayo katika mechi muhimu, hali ambayo imezua mjadala mkali miongoni mwa mashabiki wa klabu hiyo.

Bao hilo lilivuruga matumaini ya Gor Mahia ambao walitangulia kufunga mapema kupitia kwa Meddie Kagere.

Kagere ambaye alionyeshwa kadi ya njano kwa mara ya pili ataikosa mechi hiyo.

Kwingineko, beki wa Harambee Stars David Owino Jumamosi alifunga bao lake la kwanza katika mashindano ya bara  akiwajibikia timu yake ya Zesco United katika kipute cha kuwania klabu bingwa barani Afrika.

Zesco United ilikuwa ikichuana na Mbabane Swallows kutoka Swaziland kipute kilichoishia sare ya 1-1 ugani Levi Mwanawasa eneo la Ndola nchini Zambia.

Beki huyo wa zamani wa Gor Mahia alitia wavuni bao hilo muhimu katika dakika ya 65 huku wapinzani wao wakibahatika kuona lango zikiwa zimesalia dakika kumi mechi ikamilike.

Katika matokeo mengine vigogo wa soka barani Al Ahly kutoka Misri na Esperance kutoka Tunisia walitoshana nguvu kwa sare tasa katika mechi ya kwanza ya kundi A iliyogaragazwa juzi.

Minnows Township Rollers ya Uswazi walionyesha Kampala City kutoka nchi jirani ya Uganda vimulimuli kwa kuwapokeza kichapo chembamba cha 1-0 na kuchukua uongozi wa mapema wa kundi A.

Kundi B ilishuhudia TP Mazembe kutoka Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wakichukua uongozi baada ya kuwabamiza wapinzani wao Entente Setif kutoka Algeria mabao 4-1.

Timu nyingine katika kundi hilo Moulodia Alger kutoka Algeria na Difaa el Jadida ya Morocco ziliagana sare ya 1-1.

Katika matokeo mengine ya makundi, WAC Casablanca ambao ni mabingwa watetezi wa kombe hilo waliagana sare ya 1-1 na Mamelodi Sundowns kisha Togo Port wakakalifishwa 2-1 na Klabu ya Horoya kutoka Guinea.

Michuano ya mwaka huu inatarajiwa kunoga zaidi kwa sababu timu ambazo zinashiriki zimeonyesha nia ya kuwa wagombezi halisi na zinatarajia kumaliza ubabe wa miaka mingi wa klabu za Esperance, Al Ahly, TP Mazembe na WAC Casablanca.

You can share this post!

OBARA: Serikali isibadili sembe bila ruhusa ya raia wake

Kitambi atajwa kocha bora wa mwezi KPL

adminleo