• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 7:55 AM
Pwani yaapa kujisuka upya kuingia serikalini 2022

Pwani yaapa kujisuka upya kuingia serikalini 2022

Na KAZUNGU SAMUEL

VIONGOZI wa Pwani wanapanga kuungana na kuwa katika serikali mwaka wa 2022 na wakapendekeza kuwa Gavana wa Kilifi, Amason Kingi aongoze kampeni hiyo.

Wengi wakiwa wanasiasa, walisema Jumamosi wakati wa mazishi ya waliyekuwa mbunge wa Ganze, marehemu Joseph Kingi kwamba wameanza harakati za kutimiza azimio la umoja wa Pwani.

Gavana Kingi aliwataka wanasiasa wakongwe na viongozi wa kidini kuhakikisha azimio la umoja wao linafanikiwa.

“Ikiwa mimi niko tayari, mwingine pia awe tayari na mwingine vile vile. Tukifanya hivyo kama wakazi wote wa Pwani, basi lengo letu la kuwa katika serikali tukiwa kitu kimoja litafaulu,” akasema Gavana Kingi.

Mazishi hayo yalifanyika katika kijiji cha Mitsemerini, Bamba na kuhudhuriwa na miongoni mwa wengine, mkuu wa majeshi Jenerali Samson Mwathethe.

Viongozi hao ambao walikuwa ni wabunge wa sasa na wa zamani, walisema maeneo mengine ya Kenya yanaheshimiwa kwa kuwa viongozi wote wanaongea kwa sauti moja.

Mbunge wa Kaloleni, Bw Paul Katana alisema kuna haja ya kuwa na msimamo kati ya wakazi wa Pwani na viongozi wao ili kutoyumbishwa katika siasa.

“Mara hii tunataka kuwa katika nyumba yetu. Hii tabia ya kushika nyumba za wengine haitatusaidia.

Tunashukuru kwamba baada ya Bw Raila Odinga na RaisUhuru Kenyatta kushikana mikono, kile ambacho  tumeona sasa ni utulivu wa nchi. Lazima tufurahie hatua hii ambayo viongozi wetu walichukua,” akasema Bw Katana.

Wanasiasa wengine walikuwa Teddy Mwambire (Ganze), Ken Chonga (Kilifi Kusini), Asha Jumwa (Malindi), Owen Baya (Kilifi Kaskazini) na Mwakilishi wa akina mama wa Kaunti Bi Mbeyu Mwanyanje.

Waliowahi kuwa wabunge ni pamoja na Gunga Mwinga, Abdalla Ngozi, Francis Baya, Morris Dzoro, Katana Ngala na Gonzi Rai.

Bw Mwambire alisema kuwa umoja wa viongozi wa Pwani umetatizwa mara nyingi na chuki pamoja na masengenyo na wivu miongoni mwa viongozi wenyewe.

 

Kuimarisha umoja

“Tunataka sasa kuhakikisha kwamba tunatimiza lengo kamili la umoja wetu. Lakini tatizo linakuja wakati ambapo chuki huanza kuwaingia viongozi na kuanza kupigana vita, kuchongeana na kubezana. Wakati tukiacha hili, basi tutafanikisha azimio letu la umoja,” akasema.

Naye Bi Jumwa alisema kuwa tayari eneo hilo liko na umoja lakini kinachosumbua ni kuwa bado hakujapatikana kiongozi ambaye ataweza kuwaleta pamoja kama Wapwani.

“Gavana Kingi yuko hapa lakini tatizo letu ni kuwa kila kiongozi ambaye anajitokeza kutaka kutupeleka mbele anapingwa. Hili ni tatizo kubwa kwetu na ni lazima tubadilike,” akasema Bi Jumwa.

Bw Owen alisema gavana anatosha kuchukua usukani kama kiongozi wa Pwani na kuwapeleka katika serikali mwaka wa 2022.

Aliyekuwa mbunge wa Kaloleni Bw Gunga pia alisema eneo la Pwani linatatizika kwa sababu halina viongozi ambao wanaweza kusukuma sera za eneo hilo kitaifa.

“Lazima tupate kiongozi ambaye atatushika mkono kama Pwani na kutuweka pamoja katika mizani ya maendeleo,” akasema.

 

You can share this post!

Mwili wa mwanamke aliyetoweka wapatwa umezikwa shambani

Mabadiliko ya sheria ya SRC yaibua hofu

adminleo