• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 6:55 PM
Aibu duniani wanariadha Wakenya wakizidi kutumia pufya

Aibu duniani wanariadha Wakenya wakizidi kutumia pufya

Na CHRIS ADUNGO

BINGWA wa zamani wa dunia katika mbio za mita 1,500 Elijah Manangoi, 27, ni miongoni mwa wanariadha wanne wa Kenya ambao wameadhibiwa na Kitengo cha Maadili (AIU) cha Shirikisho la Riadha Duniani (IAAF) kwa kukiuka kanuni zinazodhibiti matumizi ya pufya.

Watatu wengine ambao wamepigwa marufuku ni Patrick Siele, Kenneth Kiprop Kipkemoi na Mercy Jerotich Kibarus ambao ni watimkaji wa marathon.

Baada ya kuibuka mfalme wa dunia mnamo 2017, Manangoi alitawala Michezo ya Jumuiya ya Madola na mbio za Bara la Afrika mnamo 2018. Anajivunia pia kushinda mbio za mita 1,500 kwenye duru mbalimbali za Wanda Diamond League katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 27 amesimamishwa kwa muda na AIU kwa hatia ya kutojiwasilisha kwa minajili ya kufanyiwa vipimo vya afya ili kubaini iwapo alitumia dawa za kusisimua misuli au la. Kwa mujibu wa kanuni za Shirika la Kukabiliana na Pufya Duniani (WADA), mwanariadha anayekosa kufanyiwa vipimo mara tatu chini ya kipindi cha miezi 12, hupigwa marufuku moja kwa moja.

Siele, 24, amesimamishwa kwa muda kwa kosa la kukwepa na (au) kutojiwasilisha kwa minajili ya vipimo vya afya mara tatu mfululizo. Muda wake bora zaidi katika mbio za marathon ni saa 2:10:42 aliouandikisha katika Shanghai International Marathon mnamo 2019. Aliambulia nafasi ya sita katika mbio hizo.

Huku Manangoi na Siele wakisimamishwa kwa muda kwenye ulingo wa riadha, Kipkemoi na Kibarus wamepigwa marufuku ya vipindi virefu baada ya chembechembe za dawa haramu aina ya Terbutaline na Norandrosterone kupatikana katika sampuli zao za damu.

Kipkemoi sasa atakuwa nje ya ulingo wa riadha kwa miaka miwili huku marufuku yake yakianza kutekelezwa rasmi mnamo Februari 25, 2020. Matokeo yote katika mbio alizozishiriki tangu Septemba 12, 2019 pia yamefutiliwa mbali.

Mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 35 aliambulia nafasi ya pili kwenye Michezo ya Afrika mnamo 2011 nchini Msumbuji kabla ya kuibuka mshindi wa NN Rotterdam Marathon nchini Uholanzi mnamo 2018. Alikamilisha mbio za mita 10,000 kwenye Riadha za Dunia zilizoandaliwa jijini London, Uingereza mnamo 2017.

Kwa upande wake, Kibarus, 36, amepigwa marufuku ya miaka minane ambayo yaanza kutekelezwa rasmi mnamo Disemba 5, 2019. Matokeo yote ya mbio alizonogesha tangu Septemba 13, 2019 yamefutiliwa mbali. Kibarus aliibuka mshindi wa Sydney Marathon mnamo 2018.

You can share this post!

‘Serikali imefumbia macho magonjwa mengine...

Man U wabanwa na West Ham

adminleo