• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 6:55 AM
Binti akasirisha baba kwa kuamua kumpinga kisiasa

Binti akasirisha baba kwa kuamua kumpinga kisiasa

Na DAILY MONITOR

HUKU joto la uchaguzi likiendelea kupanda nchini Uganda, mwanasiasa mmoja amemuasi bintiye aliyetangaza azma ya kumpinga katika kinyang’anyiro cha wadhifa wa uenyekiti wa Baraza la Mji wa Kasaali.

Bw Godfrey Kimera ambaye ni mwenyekiti wa Baraza la Mji wa Kasaali, wilayani Kyotera, alitaja uamuzi wa bintiye, Reginah Nakiweewa, kuwania kiti hicho kama kitendo cha utovu wa heshima kwake.

Alisema bintiye angewania kiti kingine katika uchaguzi huo, wa mwaka ujao, badala ya kiti hicho anachokishikilia wakati huu.

“Nimemshauri (Nakiweewa) mara kadha ajiondoe katika kinyang’anyiro cha kiti cha uenyekiti wa baraza la mji lakini amekataa. Siwezi nikamvumilia binti kama huyo ambaye hana heshima kwa wazee. Atafute baba mwingine,” Bw Kimera akasema kwa hasira.

Lakini Bi Nakiweewa anasema babake, ambaye ni mwanachama wa chama cha Democratic Party (DP), aliahidi kutowania kiti hicho baada ya kuhudumu kwa mihula miwili. Hii ni baada yake kuchaguliwa kwa mara ya kwanza katika uchaguzi wa 2011.

Wakati huo Kasaali ilikuwa kaunti ndogo lakini ikapandishwa hadhi kuwa baraza la mji mnamo Julai 2017 baada ya Kyotera kutangazwa kuwa wilaya.

“Nilipokuwa mdogo babangu alikuwa akituambia kuwa sisi ndio viongozi wa kesho. Sasa nimekomaa na niko tayari kuchukua usukani kutoka kwake,” Bi Nakiweewa akasema kwenye mahojiano na wanahabari.

“Yeye (Kimera) pia ndiye mmoja wa wale ambao husema Rais Museveni ameongoza kwa muda mrefu na anapaswa kuwapisha viongozi vijana. Je, anataka pia kufuata mkondo huo wa Rais Museveni?” akauliza.

Bi Nakiweewa mwenye umri wa miaka 30 alisema hatavunjwa moyo na vitisho kutoka kwa babake akisisitiza kuendelea na mipango yake ya kuwania kiti hicho.

Anapanga kuwania kiti cha uenyekiti wa Baraza la Mji wa Kasaali katika uchaguzi mkuu wa Januari 2021 kwa tiketi ya chama cha Justice Forum (JEEMA).

“Sina uhasama wowote na Bw Kimera kama mtu binafsi. Atasalia kuwa babangu. Nia yangu ni kuondoa yule mtu ambaye amefeli kutimiza ahadi zake,” akasema.

Katika kisa kingine sawa na hicho, Bw Paul Ssekandi, mwanahabari wa kujitegemea Wilayani Lyatonde, pia ametofautiana na mjomba wake, Bw Elia Ssewandigi.

Hii ni baada ya mwanahabari huyo kutangaza nia ya kushindania kiti kimoja cha kisiasa na Bw Ssewandigi katika uchaguzi mkuu wa 2021.

“Nilinunua mbwa wa kiume mapema mwezi huu na nikampa jina Paul….. Nilikuwa wa kwanza kutangaza azma ya kuwania kiti hicho (uenyekiti) na nitamshinda,” Bw Ssewandigi akasema.

Bw Ssewandigi na Ssekandi watashiriki kinyang’anyiro cha uenyekiit wa Baraza la Mji wa Lyantonde pamoja na mshikilizi wa wadhifa huo sasa Bw Mustapha Kalule.

You can share this post!

Kanuni za kuchinja Siku ya Idd kubwa

JAMVI: Je, ni busara kwa Kalonzo kuungana na Jubilee?

adminleo