• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Madaktari wa Cuba kutua nchini Mei 28 kuhudumia wagonjwa mashinani

Madaktari wa Cuba kutua nchini Mei 28 kuhudumia wagonjwa mashinani

Na CECIL ODONGO

WIZARA ya Afya Jumatatu ilitia saini makubaliano kati yake na Baraza la Magavana kuhusu ushirikiano wa kiafya na kuweka mpango mahususi kuhusu jinsi madaktari 100 wataalam kutoka nchi ya Cuba watakavyohudumu hapa nchini.

Waziri wa Afya Sicily Kariuki alisema Madaktari hao ambao watahudumu kwa kandarasi ya miaka miwili, wanatarajiwa kutua hapa nchini tarehe 28 mwezi huu na kupelekwa kaunti mbalimbali ili waanze kutoa huduma katika hospitali mbalimbali.

Bi Kariuki alisisitiza kwamba kwa kuwa sekta ya afya iligatuliwa hawakuwa na jingine ila kuwashirikisha baraza la magavana katika mpango huo na kuongeza kwamba serikali kuu imehakikisha madaktari wote 100 wanaumilisi wa lugha ya Kiingereza ili kurahisisha mawasiliano kati yao na wenzao nchini.

Kulingana na waziri huyo madaktari 50 kutoka hapa nchini pia wanatarajiwa kusafiri hadi Taifa la Cuba kwa mafunzo spesheli ya kitaaluma katika mpango maalum wa kubadilishana ujuzi kati ya Kenya na Cuba mwezi Septemba mwaka huu.

“Bodi yetu imewakagua madaktari wote 100 kutoka Cuba na tumethibitisha wanauelewaji mpana wa lugha ya Kiingereza. Pia madaktari wetu 50 watasafiri hadi India kwa mafunzo ya kipekee ya ubadilishanaji wa ujuzi wa kitaaluma baadaye Septemba,” akasema Bi Kariuki.

Madaktari hao wanatarajiwa kutoa huduma spesheli na kupunguza idadi ya wagonjwa wanaosafiri kutoka mbali kupata huduma spesheli za kiafya katika hospitali ya Kenyatta na ile ya rufaa ya Moi.

Hata hivyo hatua ya madaktari hao kuajiriwa kwa kandarasi hapa nchini imezua pingamizi kubwa kutoka kwa viongozi wa Chama cha cha Madaktari nchini(KMPDU) ambao wamesisitiza kwamba serikali kwanza ingewapa ajira madaktari 1200 wa hapa kabla haijawaleta wengine kutoka Cuba.

Katibu Mkuu wa KMPDU Dkt Ouma Oluga amekuwa katika mstari wa mbele kupinga hatua hiyo ya serikali akisema Kenya ina madaktari wataalam wa kutosha ila tu serikali haiwathamini na haitaki kuwapa kazi.

Majuzi Dkt Oluga alilalamika kwamba serikali imeonyesha kutowajali madaktari nchini kwa kujishughulisha na kuwaleta wa nje na kufumbia macho mgomo unaoendelea wa wahadhiri ambao madaktari wanachama wa KMPDU wanashiriki.

You can share this post!

Sina tamaa ya hela, asema bondia Benson Gicharu baada ya...

Ingwe yawinda mshambuliaji wa Nzoia Sugar

adminleo