• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 11:05 AM
Serikali yatisha kuwapiga kalamu madaktari wagonjwa wakizidi kuteseka

Serikali yatisha kuwapiga kalamu madaktari wagonjwa wakizidi kuteseka

BENSON MATHEKA, DIANA MUTHEU, TITUS OMINDE na LEONARD ONYANGO

HUDUMA za matibabu ziliendelea kukwama katika hospitali za umma kote nchini jana, na kuacha wagonjwa wakizidi kutekesa, huku maafisa wa serikali na wahudumu wa afya wanaogoma wakilaumiana.

Maafisa wa Wizara ya Afya wanasisitiza kuwa madaktari hawafai kugoma, wakisema wametimiziwa matakwa yao. Kulingana na Waziri Mutahi Kagwe, madaktari wamelipwa mishahara yao na hawafai kuhadaa Wakenya.

Siku ya Jumatatu wakati wa mazishi ya Dkt Stephen Mogusu katika Kaunti ya Kisii, maafisa wa Chama cha Matabibu na Madaktari wa Meno (KMPDU) walisema baadhi ya madaktari hawajalipwa mishahara yao kwa miezi kadhaa.

Jana, hata hivyo, Bw Kagwe alisema ingawa mishahara ilicheleweshwa hakuna daktari anayedai malipo.

Waziri alisisitiza kuwa madaktari wanaogoma wanafaa kufutwa kazi, kauli ambayo magavana wanakubaliana nayo. “Hatuwezi kuacha wagonjwa wakiteseka,” akasema Bw Kagwe.

Miongoni mwa matakwa ya madaktari ni bima ya matibabu na maisha, vifaa vya kuwakinga dhidi ya maambukizi ya janga la Covid-19 wakiwa kazini na kupandishwa cheo.

Naibu Waziri wa Afya Dkt Mercy Mwangangi alisema matakwa saba kati ya tisa yametimizwa.“Kilichobaki na ambacho kinashughulikiwa ni marupurupu,” akaeleza.

Waziri Kagwe alifafanua kwamba kile madaktari wanataka ni kudumishwa kwa marupurupu ambayo walipewa wakati janga la Covid-19 lilipoanza.

Hata hivyo, wahudumu wa afya walilaumu serikali na magavana kwa kutojali maslahi yao. Jana, Gavana wa Kisumu Profesa Peter Nyong’o aliunga mkono kauli ya Waziri Kagwe kwamba madaktari waliolemaza huduma katika hospitali za umma watafutwa kazi.

Katika Kaunti ya Mombasa, wahudumu waliomlaumu Gavana Hassan Joho kwa kuwapuuza, huku wakisisitiza kuwa wataendelea na mgomo hadi watendewe haki.

Wakizungumza baada ya kuandamana hadi nje ya majengo ya ofisi za Bw Joho, wahudumu hao wa afya walimtaka gavana ashughulikie malalamishi yao haraka iwezekanavyo.

“Mara nyingi tumemuona gavana wetu akitilia maanani mambo ya siasa, lakini tunapokuwa na changamoto katika sekta ya afya huwa hajitokezi kwa mazungumzo,” alihoji Mwenyekiti wa Chama cha Wauguzi Nchini (KNUN), Bi Miriam Mbithe.

Kupitia kwa viongozi wao, wahudumu hao zaidi ya 850 walisema vitisho havitawazua kuendeleza mgomo wao kitaifa ulio katika wiki ya tatu.

“Hatuogopi kufutwa kazi. Zaidi, hatutaki kufanya kazi katika mazingira yanayohatarisha maisha yetu, na katika sekta inayopuuza malalamishi ya wafanyakazi wake,” akaeleza Katibu wa Chama cha Kutetea Haki za Matabibu (KUCO) Kaunti ya Mombasa, Bw Franklin Makanga.

Wahudumu wa afya 800 Uasin Gishu walilaumu serikali ya Gavana Jackson Mandago kwa kutowapandishwa vyeo kwa miaka zaidi ya kumi, licha yao kuhitimu.

Mwenyekiti wa KNUN tawi la Uasin Gishu, Bw Francis Chepkwony, alikanusha madai kwamba shughuli za kawaida za matibabu ziliendelea katika hospitali za kaunti hiyo

.“Wanaodanganya eti huduma za afya zinaendelea katika kaunti hii wanawakejeli wakazi maskini wanaotegemea vituo vya afya vya umma kwa matibabu,” akasema Bw Chepkwony.

Gavana Mandago ni mmoja wa magavana ambao wamewapuuza wafanyikazi wa afya kwa gharama ya shughuli ambazo haziongeza thamani kwa wakaazi wa kaunti hii,’ akaongeza.

You can share this post!

Aina mpya ya corona hatari zaidi yapatikana Uingereza

MARY WANGARI: Viongozi wa kike waheshimiwe, taasubi za...