• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
FUNGUKA: Sihitaji urembo kunyaka wahadhiri chuoni na kuwalambisha asali nipite mitihani

FUNGUKA: Sihitaji urembo kunyaka wahadhiri chuoni na kuwalambisha asali nipite mitihani

Na Pauline Ongaji

Ni ndoto ya kila mwanafunzi wa chuo kikuu kufanya vyema katika mtihani wake na hata kuhitimu.

Na ni ndoto ambayo Valerie anaifuata kwa udi na uvumba na ananuia kuitimiza. Hata hivyo tofauti na wanafunzi wengine wa kawaida wanaotia bidii kimasomo kuafikia ndoto hii, binti huyu anayesomea shahada ya uzamili katika masuala ya kibiashara katika chuo kikuu kimoja hapa nchini amebuni mbinu kunufaika.

Sawa na msemo wa Kiingereza “The end justifies the means,” Valerie hajali atakachofanya kiwe kibaya au kizuri, mradi apate matokeo anayotaka. Mbinu ya binti huyu ni kuwanasa wahadhiri ili wamdokezee kuhusu maswali kwenye mtihani kabla siku yenyewe.

Kwanza kabisa binti huyu mwenye umri wa miaka 33 sio wale mabinti ambao kwa viwango vya kawaida unaweza waita warembo sana. Valerie sio mmojawapo wa mabinti wanaojirembesha. Kwa hivyo ni kawaida kukutana naye akiwa ameachilia shungi la nywele na ni nadra kwake kujipaka vipodozi.

Badala yake amewekeza nguvu na rasilmali zake kwingineko.

“Nimenoa akili yangu kiasi cha kwamba hilo ndilo lango la kwanza ninalotumia kunasa windo langu kabla ya kuliingiza katika mtego wa mahaba.

Kwangu urembo ni mchuuko sana. Mtu yeyote anaweza kuwa mrembo. Siku hizi kwa mapeni kadha ya kununua vipodozi ghali na nywele za kubandika waweza shindania tuzo ya ‘slay queen’.

Nawe ukiwa hivi, ni vigumu kwa mhadhiri kukuchangamkia na kuwa na makini kwako kwani kuna wengi kama wewe. Ukishamuonjesha, basi ni hivyo anasonga na kumwendea mpumbavu mwingine kama wewe.

Badala yake nimewekeza katika akili yangu, rasilmali ya kipekee ya kuwanasa hawa wahadhiri ambao ni ada kwao kunipa alama za juu kwenye mtihani. Badala ya kununua nywele za kubandika, mimi hutumia pesa zangu kununua vitabu na kuhakikisha kuwa nahudhuria mihadhara yote muhula unapoanza.

Kadhalika mimi hufuatilia mada kuu za kimasomo kabla ya mhadhiri kuingia, kumaanisha kuwa anapoingia kufunza mimi, ni mmojawapo wa wanafunzi wachache wanaochangamkia maswali, mbinu ambayo imenisaidia kunasa wahadhiri wengi, hasa wanaovutiwa na akili ya binti badala ya masuala sahili kama vile sura na umbo la kupendeza.

Lakini mtego wangu haukomei hapo tu kwani nimehifadhi uhondo pindi nikishawakaribisha kwenye ubongo wangu ambao ni sawa na sebule ya nyumba.

Sawa na mgeni maalum, akishaingia ukumbini lililosalia ni kumvuta hadi chumbani ambapo pia nimehakikisha kuwa kibuyu cha asali kimehifadhiwa vilivyo, na nakuhakikishia kuwa pindi anapoonjeshwa sitatumia nguvu nyingi kumshawishi ashughulikie masuala yangu wakati wa mtihani.

Nilianza tabia hii nilipokuwa nikisomea shahada yangu ya kwanza ambapo katika mtihani wa mwaka wa kwanza, licha ya kutia bidii, kuna mabinti wazembe waliofanya vyema zaidi yangu kutokana na uhusiano waliokuwa nao na wahadhiri.

Natarajia kukamilisha masomo yangu mwisho wa mwaka huu ambapo tayari nishapita katika masomo ya nadharia na katika tasnifu ninayoandika kuna ishara kubwa kuwa nitapata alama ya A.

Pia najiandaa kuanza kusomea shahada ya uzamifu pindi baada ya kukamilisha masomo na mtindo utakuwa huo huo hadi mwisho”.

You can share this post!

PAMBO: Yaliyopita yasiwe ndwele kwako

URUSI 2018: Mastaa watakaonogesha dimba

adminleo