• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:50 AM
Aliyechaguliwa kwa ODM atangaza kuwania kwa Jubilee 2022

Aliyechaguliwa kwa ODM atangaza kuwania kwa Jubilee 2022

Na Magati Obebo

NAIBU Gavana wa Kaunti ya Kisii, Joash Maangi ametangaza kuwa atawania ugavana wa kaunti hiyo kupitia chama cha Jubilee ifikapo 2022.

Mnamo Jumatatu, Bw Maangi alimwambia Naibu Rais William Ruto kuwa yuko ODM kwa muda tu na kuwa ameanzisha safari ya kurudi Jubilee.

Akiongea mjini Nyamiria, Bw Maangi alisema ana uhusiano wa karibu sana na chama cha Jubilee licha ya kuwa upinzani.

“Ningetaka kukuambia naibu rais kuwa sina amani moyoni kuwa katika upinzani. Wakati ukifika nitajiunga nawe katika chama tawala na kukufanyia kampeni za kuwa rais,” Bw Maangi alimwambia Bw Ruto wakiwa eneo la Rigoma, Kaunti ya Nyamira.

Bw Ruto alikuwa katika ziara ya siku moja eneo hilo kwa mwaliko wa wabunge Shadrack Mose (Kitutu Masaba) na Joash Nyamoko (Mugirango Kaskazini).

Viongozi hao waliapa kumuunga mkono naibu rais katika kampeni za urais ifikiapo 2022.

Mwaka jana Bw Maangi alijiunga na Jubilee kabla ya kujiunga tena na ODM akidai mawimbi ya upinzani yalikuwa mazito Kisii na huenda yangemmeza kisiasa.

Alisema hatua yake ya kurejea ODM ilitokana na ushauri kutoka kwa viongozi pamoja na wakazi wa Kaunti ya Kisii.

Bw Maangi alipokelewa tena chamani na kinara wa ODM Raila Odinga na kuahidiwa kusalia naibu gavana wa Kaunti ya Kisii baada ya uchanguzi wa Agosti 2017.

Alipojiunga na Jubilee mnamo 2015, Bw Maangi alipanga kutumia chama hicho kumng’oa Gavana James Ongwae lakini akashawishiwa na wakuu wa Jubilee kutoa nafasi hiyo kwa Chris Obure ambaye alibwagwa na Ongwae katika uchaguzi wa Agosti 2017.

You can share this post!

Viongozi wakashifu mauaji ya polisi na utovu wa usalama...

Msako mkali Nakuru baada ya wakazi kulishwa paka

adminleo