Arsenal mabingwa wa Ligi Kuu baada ya Man City kulazimishiwa sare
MIAMBA Arsenal wameibuka mabingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) baada ya washindani wao wakuu, Manchester City kulazimishiwa sare na vidume FC Bournemouth.
Baada ya miaka 22 ya ukame, kibaridi na kejeli kutoka kwa watani wao, The Gunners hatimaye wamefaulu kujinasia taji hilo la msimu wa 2025-26 Jumanne usiku pale vigogo wa muda mrefu Man City walipokosa kujipatia ushindi dhidi ya The Cherries ambao nao walikuwa wanafukuzia angalau alama moja ili wafaulu kushiriki kombe la Uefa Conference Cup msimu ujao.
Man City walikuwa nyuma ya Arsenal kwa alama tano wakienda ugani Vitality baada ya vijana wa kocha Mikel Arteta kutekeleza jukumu lao kwa kunyuka Burnley Jumatatu.
Sare ya 1-1 baina ya City na Bournemouth inamaanisha kwamba wakiwa na alama 78 dhidi ya 82 za Arsenal jedwalini, alama za juu zaidi wanazoweza kupata ni 81 kwenye mechi ya funga msimu hata kama Arsenal watapoteza dhidi ya Crystal Palace Jumapili.
Ugani Vitality Stadium, Bournemouth walicheza kwa ujasiri mkubwa dhidi ya silaha kali za Cityzens. Walikimbilia kila mpira, wakamenyana kwa ukakamavu mkubwa ambao ulionyesha sababu ya wao kucheza mechi 16 bila kupoteza mwaka huu.
Kijana Eli Junior Kroupi alifaulu kuiweka Bournemouth kifua mbele kwa bao safi dakika ya 38 baada ya mchezo na pasi za upesi zilizopumbaza safu ya ulinzi ya vijana wa kocha Pep Guardiola. Baada ya hapo ikawa ni mashambulizi baada ya mashambulizi vijana wa kocha AndroniĀ Iraola wakikosa nafasi mbili za wazi kabisa dakika za lala salama kufanya mambo kuwa 2-0.
Hata hivyo, katika muda wa majeruhi, mkali wao Erling Haaland alifaulu kunyuka bao la kusawazisha wakati safu ya ulinzi ya Bournemouth iliposhindwa kuondosha mpira kutoka eneo hatari.
Sare ya 1-1 ilimaanisha kwamba Man City hawawezi kufikia Arsenal ikiwa imesalia mechi moja msimu kukamilika na kwa hivyo kuwapokeza mashabiki wa Arsenal sherehe ya kukata na shoka.