Habari za Kitaifa

Kilichosababisha OCS wa kituo cha Central kukamatwa wakati wa maandamano

Na KAMORE MAINA, STEVE OTIENO May 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SAFARI ya kilomita 45 ya Dishan Angoya kutoka Thika Aprili 30, 2026 ilionekana kuwa kilele cha juhudi zake za kazi alipoteuliwa kusimamia moja ya vituo vikubwa na vyenye shughuli nyingi zaidi nchini, Kituo cha Polisi cha Central Nairobi.

Kwa kuwa alikuwa OCS kwa mara ya kwanza, uteuzi huo ulionekana kama hatua kubwa ya kikazi, hasa ikizingatiwa kuwa vituo vya aina hiyo huongozwa na maafisa wenye uzoefu zaidi.

Hata hivyo, wiki tatu tu baada ya kuanza kazi, sekta ya uchukuzi ilitangaza mgomo uliosambaa nchini kote kushinikiza kupunguzwa kwa bei ya mafuta.

Baadhi ya wananchi walijitokeza barabarani kupinga hali hiyo, ingawa mkuu wa polisi wa Kaunti ya Nairobi Issa Mohamud alisisitiza kuwa maandamano hayo yalikuwa haramu.

Katika machafuko hayo, watu 710 walikamatwa nchini kote, wakiwemo washukiwa wa maandamano na wengine waliodhaniwa kuwa wahalifu.

Katika Kaunti ya Nairobi pekee watu 189 walikamatwa, ambapo 64 walizuiliwa katika kituo cha Central.

Miongoni mwao walikuwa wanaodaiwa kumshambulia Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Nairobi, Issa Mohamud, aliyeshambuliwa eneo la Kangemi alipokuwa akifuatilia maandamano na kulazimika kulazwa hospitalini.

Hata hivyo, kabla ya kumaliza zamu yake, OCS Angoya alitoa amri washukiwa hao 64 waachiliwe huru, hatua iliyozua taharuki kubwa katika uongozi wa polisi.

Baada ya saa sita usiku, maafisa wa polisi walifika nyumbani kwa Bw Angoya na kumkamata.

Kwenye mlango wake, alikutana na Naibu Kamanda wa Polisi wa Kanda, Daniel Chacha, aliyemjulisha kuhusu kukamatwa kwake kwa madai ya matumizi mabaya ya ofisi na kupokea rushwa ili kuwaachilia washukiwa.

Kwa mujibu wa kanuni za polisi, maafisa wa cheo cha Angoya hawawezi kukamatwa na wasaidizi wao, ndiyo maana uongozi wa juu ulilazimika kuhusika.

Wachunguzi pia walisema Bw Angoya hakuwa na mamlaka ya kuwaachilia baadhi ya washukiwa kwa kuwa waliletwa na Idara ya Upelelezi (DCI), na si maafisa wa kituo chake pekee.

Wizara ya Masuala ya Ndani ilithibitisha kuwa baadhi ya walioachiliwa walihusishwa na shambulio dhidi ya Bw Mohamud, na ikasisitiza umuhimu wa kulinda haki na usalama kwa wote.

Sasa, OCS huyo mpya anakabiliwa na uchunguzi wa kinidhamu ambao unaweza kusababisha kufutwa kazi endapo atapatikana na hatia.