DR Congo yatikisa historia, sasa yakutana na Uingereza Senegal nao kuvaana na Ubelgiji
Baada ya kusubiri kwa miaka 52, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imeandika ukurasa mpya katika historia yake kwa kutinga awamu ya 32 bora kwa mara ya kwanza.
Mara ya mwisho taifa hilo lilishiriki Kombe la Dunia ilikuwa 1974, ambapo ilipoteza mechi zote tatu za makundi, ikiwemo kipigo cha 9-0 kutoka Yugoslavia.
Licha ya hilo, Wakongo wanaamini safari yao ya kihistoria bado haijafika mwisho. Ushindi dhidi wa 3-1 dhidi ya Uzbekistan uliowavusha kutoka hatua ya makundi umeongeza imani kambini, na sasa matumaini yao ni kuendeleza maajabu dhidi ya Uingereza.
Ubelgiji na Senegal nao watavaana katika Uwanja wa Seattle, huku kila upande ukiamini unaweza kuendelea na safari ya kusaka ubingwa.
Ubelgiji imeonyesha sura mbili tofauti kwenye mashindano haya. Ilianza kwa sare tasa dhidi ya Iran kabla ya kutoka sare ya 1-1 na Misri na kufufuka na kuichapa New Zealand 5-1.
Kwa upande wa Senegal, matokeo yamekuwa mseto. Simba wa Teranga walifungwa 3-0 na Ufaransa, wakapokea kichapo kingine cha mabao 3-1 kutoka Norway, lakini wakamaliza hatua ya makundi kwa kishindo kwa kuifunga Iraq 5-0.
Katika mechi nyingine, Mexico itakutana na, baada ya kumaliza hatua ya makundi bila kupoteza hata mchezo mmoja.
Chini ya kocha Javier Aguirre, wenyeji hao wamekuwa miongoni mwa timu zilizovutia zaidi kwenye mashindano haya. Waliongoza Kundi A kwa alama tisa kamili, wakifunga mabao sita na kutoruhusu hata bao moja wavuni mwao.
Ecuador haitakuwa mpinzani wa kudharauliwa. Wametinga hatua hii baada ya kuandika moja ya matokeo ya kushangaza zaidi katika hatua ya makundi kwa kuifunga Ujerumani 2-1, ushindi uliowapa tiketi ya kuendelea kama moja ya timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu.
Mabingwa wa 2018, Ufaransa, watakabiliana na Uswidi huku wakitajwa kuwa miongoni mwa timu zenye nafasi kubwa ya kutwaa taji la mwaka huu.
Les Bleus walimaliza kileleni mwa Kundi I kwa alama tisa baada ya kuzishinda Senegal, Iraq na Norway. Mbali na nahodha Kylian Mbappe, mshambuliaji Ousmane Dembele ameonyesha makali makubwa baada ya kufunga mabao matatu katika mchezo dhidi ya Norway.
Uswidi nao wameonyesha kupambana licha ya kufika hatua hii kwa taabu. Ilimaliza ya tatu katika Kundi F ikiwa na alama nne baada ya kuifunga Tunisia, kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Japan na kuchapwa 5-1 na Uholanzi.