Dimba

Morocco taifa la kwanza la Afrika kufuzu 16 bora

Na TOTO AREGE June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Morocco ilikuwa taifa la kwanza la Afrika kufuzu raundi ya 16 bora, baada ya kuiondoa Uholanzi kwa ushindi wa penalti 3-2 kufuatia sare ya 1-1 iliyodumu hadi mwisho wa dakika 120.

Mchezo ulikuwa wa kusisimua na Uholanzi walionekana kunyakua ushindi dakika ya 72 kupitia Cody Gakpo, aliyefunga baada ya shambulizi la kushtukiza na kusherehekewa na wachezaji wenzake.

Gakpo alicheza mechi hiyo licha ya kuwa katika kipindi kigumu baada ya kutangaza kufiwa na mtoto wake ambaye alikuwa bado tumboni.

Hata hivyo, Morocco hawakukata tamaa na wakasawazisha katika dakika za majeruhi kupitia Issa Diop aliyefunga kwa kichwa baada ya kupokea krosi ya Chemsdine Talbi.

Morocco sasa watavaana na Canada katika hatua inayofuata.

Mabingwa mara nne Ujerumani waliaga mashindano baada ya kulazwa 4-3 kupitia mikwaju ya penalti na kufuatia sare ya 1-1 iliyodumu hadi mwisho wa dakika 120.

Kipa Orlando Gill aliibuka shujaa wa Paraguay baada ya kuokoa penalti za Kai Havertz na Nick Woltemade, huku Jose Canale akifunga penalti ya ushindi iliyowapeleka Waparaguay hatua ya 16 Bora.

Paraguay walitangulia dakika ya 42 kupitia Julio Enciso aliyetikisa wavu kwa kichwa na kuwanyamazisha Wajerumani. Baada ya mapumziko, Ujerumani waliinuka na kusawazisha kupitia Havertz aliyemalizia kwa kichwa krosi ya Florian Wirtz.

Paraguay sasa watakutana na mshindi kati ya Ufaransa na Uswidi katika hatua ya 16 Bora.

Katika mechi nyingine, Gabriel Martinelli aliibuka shujaa wa Brazil baada ya kufunga bao la ushindi katika dakika ya 95 na kuiongoza timu hiyo kutinga hatua ya 16 Bora kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Japan.

Brazil sasa itakutana na mshindi kati ya Norway na Ivory Coast katika raundi inayofuata baada ya kuibuka kidedea katika pambano lililokuwa gumu hadi sekunde za mwisho.

Japan ndiyo waliokuwa wa kwanza kutikisa wavu dakika ya 32 kupitia Kaishu Sano.

Brazil walionekana kupoteza mwelekeo kipindi cha kwanza, lakini walirejea kwa nguvu. Kiungo mkongwe Carlos Casemiro aliisawazishia Brazil dakika ya 55 kwa kichwa baada ya kupokea krosi ya Gabriel kutoka upande wa kushoto.

Dakika za majeruhi, Bruno Guimaraes aliyepata mpira karibu na eneo la hatari la Japan na kummegea Martinelli, ambaye alitulia kabla ya kupiga shuti na kuingia wavuni, na kuwavunja mioyo Wajapani.