Dimba

Pogba alivyobubujika machozi akirejea kusakata soka baada ya kibaridi cha miaka 2

Na GEOFFREY ANENE, MASHIRIKA June 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya kupigwa na kibaridi cha kutocheza soka kwa miaka miwili, nyota wa zamani wa Manchester United na Juventus, Paul Pogba aliangua kilio kufurahia kusaini kwake kandarasi ya kuchezea AS Monaco ya Ufaransa mnamo Jumamosi.

Kiungo huyo mbunifu mwenye umri wa miaka 32 alisakata mechi yake ya mwisho Septemba 2023 akiwa Juventus kabla ya kuanza marufuku ya miezi 18 kwa hatia ya matumizi ya dawa za kusisimua misuli ambayo hata hivyo Mahakama ya Kusikiliza Mizozo ya Michezo (CAS) ilikubali “hakufanya kimaksudi”.

Mfaransa huyo mwenye asili ya Guinea mwanzoni alikuwa amepigwa marufuku miaka minne ambayo ilipunguzwa baada ya kukata rufaa na kumpa fursa ya kurejea katika soka Machi 2025.

Pogba ametia saini mkataba wa miaka miwili na AS Monaco. PICHA | MASHIRIKA

Itakumbukwa Novemba 2024, Pogba na Juventus waliamua kukatiza kandarasi yao ambayo ilifaa kutamatika 2026.

Baada ya miezi minane bila kupata klabu, Pogba hatimaye ameajiriwa na Monaco. Aliaminika pia kumezewa mate na klabu za Ligi Kuu ya Saudi Arabia na Ligi Kuu ya Amerika na Canada. Pogba amesaini kandarasi ya miaka miwili na Monaco na anatarajiwa kuvalia jezi nambari 8.

Mwanasoka huyo atashiriki Ligi Kuu ya Ufaransa kwa mara ya kwanza kabisa kwani klabu yake ya kwanza katika soka ya watu wazima ilikuwa Manchester United msimu 2011-2012. Alielekea Juve msimu 2012-2016, United 2016-2022 na Juve 2022-2024 kabla ya kunyakuliwa na Monaco.

Pogba, ambaye ajenti wake Rafaela Pimenta pia anawakilisha wachezaji matata kama Erling Haaland (Manchester City), Noussair Mazraoui (Manchester United) na Henrikh Mkhitaryan (Inter Milan) na kocha Arne Slot (Liverpool), alichezea Ufaransa mara 91 na huenda akapata fursa ya kuiwakilisha kwenye Kombe la Dunia 2026.

Chozi la furaha na pia huzuni

Ikitangaza kuwasili kwake Jumamosi, Monaco ilitoa video ya Pogba akizidiwa na hisia akisaini kandarasi.

Chozi lilianguka kwenye kandarasi alikuwa akisaini wakati alikuwa akijifuta uso na akashukuru waliohusika katika kumpa fursa tena ya kutandaza kabumbu kwa imani yao.

Katika mahojiano ya awali na TF1 mjini Monaco kabla ya kukamilisha uhamisho wake, Pogba alisema kuwa yuko tayari kiakili na kimwili na anasubiri kwa hamu kuanza upya.

“Licha ya umri wangu, bado mimi ni kama mtoto. Bado napenda kucheza na mpira, kuchenga. Nimerudi kuwa yule mtoto nilikuwa nikianza soka Roissy-en-Brie. Nawazia jinsi mambo yatakuwa kama chipukizi anayeingia katika akademia kwa mara ya kwanza. Kila kitu kitategemea na mimi mwenyewe,” akaeleza Pogba kabla ya kukosoa Juventus kwa kutomsaidia kujiweka sawa kimwili akiwa bado na kandarasi na miamba hao wa Italia.

Pogba akipasha misuli joto wakati akichezea Juventus mnamo Mei 2023. Alisuta timu hiyo kwa kukosa kusimama naye wakati wa masaibu yake ya pufya. PICHA | REUTERS

“Hawakunipa usaidizi wowote licha ya kuwa bado nilikuwa mchezaji wao…. Sikuwaelewa kwa sababu mimi sikuwa na vita nao.”

Pogba anaungana kambini mwa Monaco na wachezaji wa zamani wa Ligi Kuu ya Uingereza kama Folarin Balogun, Mika Biereth (Arsenal), Takumi Minamino (Liverpool) na Denis Zakaria (Chelsea).