Misri yaandikisha historia Kombe la Dunia
Nahodha wa Misri Mohammed Salah alisema kuwa, ushindi huo ulikuwa kistoria baada ya kufuzu raundi 16 kwa mara ya kwanza katika Kombe la Dunia.
Misri ilifuzu baada ya kuichapa Australia 4-2 kwa mikwaju ya penalti kufuatia sare ya 1-1 baada ya dakika 120. Sasa Mafarao watavaana na mshindi kati ya Argentina katika hatua inayofuata.
“Ni historia. Niliwaambia wachezaji kabla ya mechi kuwa huu ndio uwanja mkubwa zaidi wa soka duniani. Wauchezee kwa kujiamini na msikubali presha iwatawale. Nina furaha tumefanikiwa kuandika historia,” alisema Salah.
Salah alifunga penalti yake kwa ustadi mkubwa kwa njia ya Panenka kabla ya beki Hossam Abdelmaguid kufunga mkwaju wa ushindi. Kwa upande wa Australia, Harry Souttar na Lucas Herrington walikosa penalti zao.
Misri ilitangulia dakika ya 13 kupitia Emam Ashour aliyetikisa wavu baada ya kupokea krosi ya Karim Hafez. Bao hilo lilikuwa la pili kwa Ashour katika mashindano haya na kuifanya Misri kufikisha mabao sita, zaidi ya yale iliyofunga katika ushiriki wake wa awali wa Kombe la Dunia mwaka 1934, 1990 na 2018 kwa pamoja.
Australia ilitafuta bao la kusawazisha mara kadhaa lakini ikashindwa kutumia nafasi zake. Dakika ya 55, Misri ilijifunga kupitia Mohamed Hany aliyeelekeza mpira wavuni mwake baada ya krosi ya Aiden O’Neill, na kufanya mchezo huo kuwa sare ya 1-1.
Baada ya dakika 120 kushindwa kumpata mshindi, mechi iliamuliwa kwa mikwaju ya penalti ambapo Misri ilionyesha utulivu mkubwa na kuibuka mshindi.
Baada ya ushindi huo wa kihistoria, Salah alisema kuwa ndoto ya Misri ilikuwa kuandika historia.
Mabingwa watetezi Argentina walinusurika kutolewa mapema katika Kombe la Dunia baada ya kuilaza Cape Verde 3-2 baada ya muda wa ziada katika mechi ya kusisimua ya hatua ya 32 bora.
Cape Verde, ambayo inashiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza, iliwapa Argentina wakati mgumu kwa kusawazisha mabao mara mbili kabla ya kujifunga dakika ya 111 na kuipa Argentina ushindi.
Lionel Messi aliitanguliza Argentina dakika ya 29 nao Cape Verde walisawazisha kipindi cha pili. Dakika mbili baada ya muda wa nyongeza kuanza, Lisandro Martinez aliirejeshea Argentina uongozini
Hata hivyo, Sidny Lopes Cabral aliifungia Cape Verde bao la kusawazisha kwa shuti kali lililomshinda kipa Emiliano Martinez na kufanya matokeo kuwa 2-2.
Cape Verde ilikaribia kupeleka mchezo kwenye mikwaju ya penalti lakini Diney Borges alijifunga dakika ya 111 na kuihakikishia Argentina tiketi ya hatua ya 16 bora.
Colombia ilifuzu hatua ya 16 bora baada ya kuichapa Ghana bao 1-0 katika mechi iliyochezewa jijini Kansas City. Bao la pekee la mchezo lilifungwa na Jhon Arias dakika ya 14 baada ya kupokea krosi safi kutoka kwa Luis Suarez.