Pep sasa ni maombi tu!
MANCHESTER City inaendelea kujipa imani katika mbio za kufukuzia ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu licha ya washindani wao wakuu Arsenal kufungua mwanya wa alama tano juu ya jedwali.
The Citizens walikuwa wamepunguza pengo hadi alama mbili dhidi ya vinara Arsenal Jumamosi walipoibamiza Brentford 3-0 ugani Etihad.
Kikosi cha kocha Pep Guardiola kilikuwa kimeteleza Jumatatu iliyopita kwa sare ya 3-3 dhidi ya Everton, lakini wikendi hii kilijikakamua kipindi cha pili na kuwapa mashabiki wao kila sababu ya kutabasamu.
Hata hivyo, furaha yao ilidumu kwa saa 24 pekee kwa sababu The Gunners walijinyakulia ushindi mwembamba na uliosheheni gumzo kubwa dhidi ya West Ham, pale goli la kusawazisha la The Hammers lilipokataliwa na VAR na kuruhusu vijana wa Mikel Arteta kuondoka na alama zote tatu.
Jumamosi huko Etihadi, nyota wa Ubelgiji Jeremy Doku alikuwa mwiba kwa difensi ya Brentford tangu mwanzo wa mchezo.
Alikosa bao la mapema baada ya kipa Caoimhin Kelleher kuokoa shuti lake, huku pia akimpakulia krosi safi Erling Haaland ambaye alikosa kulenga shabaha.
City walitawala kipindi cha kwanza lakini wakashindwa kuvunja ukuta wa Brentford. Baadaye Haaland alipiga kichwa kilichookolewa na Kelleher kabla ya juhudi nyingine kuzuiwa na Kristoffer Ajer.
Bao la kwanza liliwadia katika dakika ya 60 wakati Doku alipopenya upande wa kushoto na kupiga shuti kali lililotinga kona ya mbali.
Haaland aliongeza la pili dakika ya 75 baada ya vurugu ndani ya eneo la hatari, huku mchezaji wa akiba Omar Marmoush akifunga la tatu katika dakika za mwisho za kipindi cha pili.
Hata hivyo, Brentford pia walikuwa mwiba katika nyakati tofauti. Kipa Gianluigi Donnarumma alilazimika kufanya kazi ya ziada kuokoa mashambulizi ya Michael Kayode na Igor Thiago.
Baada ya ushindi huo, Guardiola alisema siri ya mabao ni kuwapeleka wachezaji karibu na Haaland.
Sasa City wanaomba sana Arsenal iteleze katika mechi zilizosalia na wao washinde zao dhidi ya Crystal Palace na Bournemouth ili mbio za ubingwa ziende hadi siku ya mwisho.
Kwingineko
Katika mechi nyingine, Liverpool walilazimishwa sare ya 1-1 katika mtanange uliogaragazwa nyumbani Anfield. Ryan Gravenberch alifungia wenyeji bao mapema dakika ya sita kabla ya Enzo Fernandez kusawazishia Chelsea dakika ya 35.
Mashabiki wa Liverpool walionyesha kutoridhishwa na maamuzi ya kocha Arne Slot, hasa baada ya kumtoa kinda Rio Ngumoha kipindi cha pili.
Nao Bournemouth waliibuka na ushindi muhimu wa 1-0 dhidi ya Fulham kupitia bao la la Rayan Christie dakika ya 53, katika mechi ya vuta nikuvute iliyoshuhudia kila timu ikibaki na wachezaji 10 kufuatia kadi nyekundu za kipindi cha kwanza baada ya ukaguzi wa VAR.
Rayan Rocha alikuwa wa kwanza kutimuliwa uwanjani baada ya kuonekana kumchezea vibaya Timothy Castagne katika tukio lililothibitishwa na VAR.
Hata hivyo, Fulham nao hawakudumu na idadi kamili ya wachezaji baada ya beki Joachim Andersen kupewa kadi nyekundu kwa kosa kama hilo dhidi ya Adrien Truffert.
Ushindi huo umeimarisha matumaini ya Bournemouth kumaliza msimu katika nafasi za kushiriki michuano ya Uropa msimu ujao.
Katika mtanange mwingine, Brighton waliwanyorosha washika mkia Wolves 3-0 na kupanda hadi nafasi ya saba kwenye jedwali.
Katika uwanja wa Stadium of Light, Sunderland walitoka sare tasa na Manchester United.