Kang’ata kupiga teke UDA kwatikisa ngome, baadhi wakimkosoa kutema chombo kilichomfaidi
GAVANA Irungu Kang’ata wa Murang’a ameibuka tena kama mmoja wa viongozi wanaotikisa siasa za Mlima Kenya, baada ya kutangaza kuwa hatawania tena ugavana kwa tiketi ya UDA mwaka 2027, hatua iliyoibua mjadala mpana kuhusu mustakabali wake wa kisiasa.
Wadadisi wa siasa wanasema Kang’ata ni “twiga wa siasa” — kiongozi mwenye mtazamo wa mbali, na ambaye haogopi kusema ukweli hata ikiwa unaumiza maslahi ya walio mamlakani.
Kang’ata alithibitisha uamuzi wake wa kujiondoa kuwania tiketi ya UDA katika uchaguzi mkuu wa 2027, akisema alifikia uamuzi huo baada ya tafakari na mazungumzo ya ndani kushindwa kuleta muafaka.
“Mheshimiwa Rais amekuwa akituambia kila mara kwamba wananchi ndio wenye mamlaka ya mwisho. Nashukuru kwa kauli hiyo, na hivyo jukumu langu ni kufuata kile wananchi wamesema,” alitanguliza kwenye kikao na wanahabari Jumapili iliyopita.
“Kwa msingi huo, kwa kuwa nimejaribu kadri ya uwezo wangu kutatua masuala haya ndani ya chama, nimefanya mazungumzo ya wazi na Mheshimiwa Rais moja kwa moja, ambapo tulijadili mawazo haya lakini hatukufikia ‘muafaka kamili’,” akasema.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa hana uhasama na Rais William Ruto au UDA akieleza kuwa ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu hadi mwisho wa muhula wake.
“Hadi wakati huo nitasalia mwanachama mwenye nidhamu na aliyejitolea wa UDA. Nitaendelea kuhudumu kwa uaminifu katika wadhifa wangu na kushirikiana na serikali ya kitaifa,” akaeleza.
Kang’ata alifafanua zaidi msimamo wake wa kisiasa akisema halengi kiti kikubwa zaidi ya ugavana na kwa hivyo yeye si tisho kwa rais.
“Sina nia ya kugombea kuwa Rais wa Kenya wala sitaki kuwa Naibu Rais wa nchi. Kwa hivyo, maslahi yangu na yake hayagongani. Yangu ni kulinda kiti changu cha Murang’a pekee,” alisema.
Aliongeza kuwa bado hajachagua chama au jukwaa jipya atakalotumia mwaka 2027.
“Baada ya kutafakari kwa kina kuelekea 2027 sitatetea kiti changu kwa tiketi ya chama cha sasa. Baadaye nitatoa taarifa kuhusu jukwaa nitakalotumia kujitokeza mbele ya wapiga kura,” akaongeza.
Alidokeza kwamba amekuwa akishinikizwa kisiasa hasa wakati wa ziara za Rais katika kaunti yake.
“Nimeona kwa siku chache zilizopita, Rais amekuwa Murang’a, na kila ninapokwenda huko, ninashinikizwa kuunga mkono miradi yake,” alisema.
Kauli hizi zimezua athari za haraka ndani ya UDA, ambapo baadhi ya viongozi wa Murang’a wamemkosoa vikali.
Waziri wa Ardhi Alice Wahome na Mbunge Mary Wamaua walimshambulia gavana huyo wakisema ametema chama alichonufaika nacho kumpa kiti cha ugavana.
Lakini kwa wafuasi wake, Kang’ata ni kiongozi jasiri anayesema ukweli bila kuogopa mamlaka.
Historia yake ya kisiasa inaonyesha kwamba mara kadhaa amechukua misimamo migumu, ikiwemo kuonya hali ya Mlima Kenya kuelekea 2022 na sasa kutoa tahadhari kwa UDA kuhusu mwelekeo wake kuelekea 2027.
Katika mahojiano mengine wiki hii, Kang’ata alionyesha wasiwasi wake kuhusu mwelekeo wa siasa akisema: “Nimeona jinsi siasa zinavyoendelea, na sasa ninaamini kwamba hazitaishia vizuri kwa chama cha UDA, angalau katika eneo langu.”
Aliongeza: “Kinachonisikitisha ni kile UDA inachofanya kuhakikisha inabaki na uungwaji mkono. Nasema hivyo kwa sababu naamini kwamba kwa miaka miwili au mitatu iliyopita, kumekuwa na matendo ambayo yameimarisha upinzani.”
Kulingana na mdadisi wa siasa Dkt Isaac Gichuki, hatua ya Kang’ata sio ya kijasiri tu mbali ni ya mtu anayetazama mbali.
“Kang’ata amejisawiri kama kiongozi jasiri anayesema ukweli bila woga “twiga wa siasa” ambaye bado analenga mustakabali wa 2027 kwa macho ya mbali.
“Kilicho wazi ni kwamba Irungu Kang’ata ameendelea kujijenga kama mmoja wa viongozi wachache wanaoweza kusema “hapana” kwa mamlaka, na kubaki bado na ushawishi mkubwa wa kisiasa. Katika siasa za 2027, twiga huyu wa Murang’a bado anaonekana kuwa juu ya uwanja—akiona mbali kuliko wengine,” asema Dkt Gichuki.