Alitegwa kwa hirizi? Mwizi wa mbuzi apatwa zizini amejifunga kamba shingoni
ZHOGATO, Kilifi:
WAKAZI wa kijiji hiki walivutiwa na tukio la kiajabu ambapo mwizi wa mbuzi aliaibika kwa kupatikana akiwa amejitia kamba shingoni ndani ya zizi.
Ni kisa kinachoaminika kusababishwa na zindiko au fingo lililomnasa mwizi huyo kisawasawa.
Alikuwa amevamia zizi la mbuzi usiku wa manane madhumuni yakiwa ni kuiba.
Ila alijipata akijiingiza kamba shingoni na kujifunga mwenyewe kwenye mojawapo ya nguzo kabla ya kusubiri kwa utulivu mwingi hadi mapambazuko kupisha mwenye mbuzi kumfungulia sawa na mifugo wengine.
Kulipokucha, mwenye boma hakushangaa kumkuta jombi akiwa amejibanza zizini huku akitafunatafuna mdomoni na kutoa sauti ya mbuzi.
Mwenye boma huyo alijua fika kwamba mtego wake wa fingo ulinasa kikamilifu.
Majirani walifahamishwa na kufika mahali pale ambapo baadaye walimrai mwenye boma kumtegua jombi huyo na kumwachilia huru kwani alikuwa amepata funzo la mwaka wakiamini kuwa katu hatorudia tabia yake ya wizi maishani.