Habari

Wahuni wavamia shule Chemelil, wajeruhi wafanyakazi na walimu na kutoroka

Na DOMNIC OMBOK June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KILICHOPASWA kuwa siku ya kawaida ya wanafunzi kurejea shuleni baada ya mapumziko ya katikati ya muhula kiligeuka kuwa mkasa wa kutisha Alhamisi katika Shule ya Chemelil Sugar Academy, Kaunti ya Kisumu.

Hii ni baada ya genge la watu wenye silaha kuvamia taasisi hiyo na kuwashambulia walimu, wazazi na wafanyakazi kabla ya kutorokea katika mashamba ya miwa yaliyo karibu.

Wavamizi hao, wanaokadiriwa kuwa karibu 30, walifika shuleni humo wakati wanafunzi walikuwa wakirejea shuleni.

Wakiwa na mapanga, marungu na pinde, walidaiwa kuwashambulia walimu na wazazi, wakaharibu mali katika ofisi mbalimbali na kuiba pesa, simu za mkononi na vitu vingine vya thamani.

Mlinzi wa shule Lynus Too alisema uvamizi huo ulianza katika lango kuu la shule.

“Walinipiga mgongoni na kunilazimisha kufungua lango. Kisha wakatoboa tairi ya baiskeli yangu kabla ya kuwageukia walimu na wazazi,” alisema.