Habari

Barchok, maafisa 10 kutupwa gerezani kwa kudharau korti

Na JOSEPH OPENDA June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Bomet, Profesa Hillary Barchok, Karani wa Kaunti Simeon Mutai, mwenyekiti wa Bodi ya Utumishi wa Umma ya Kaunti pamoja na maafisa wengine wanane wakuu wa kaunti wamehukumiwa kifungo cha mwezi mmoja jela kwa kosa la kudharau amri ya mahakama.

Maafisa hao 11 walipatikana na hatia ya kudharau Mahakama ya Ajira na Mahusiano ya Kazi baada ya kushindwa kutekeleza amri iliyowataka kuwarejesha kazini wafanyakazi 30 ambao mikataba yao ya ajira ilisimamishwa kinyume cha sheria na Serikali ya Kaunti ya Bomet.

Mahakama ilibaini kuwa viongozi hao walikaidi amri ya awali iliyoagiza wafanyakazi hao warejeshwe kazini, hatua iliyosababisha kuchukuliwa kwa hatua kali za kisheria dhidi yao.

Katika uamuzi wake, mahakama iliamuru kwamba Gavana Barchok na maafisa wenzake wafungwe katika Gereza la Serikali la Nakuru kwa muda wa mwezi mmoja.

Hata hivyo, mahakama ilieleza kuwa kifungo hicho kinaweza kusitishwa ikiwa maafisa hao watathibitisha kuwa wametekeleza kikamilifu amri ya mahakama ya kuwarejesha wafanyakazi hao kazini.