• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 11:55 AM
Asema mume alifaa kufa badala ya mbwa

Asema mume alifaa kufa badala ya mbwa

Na MASHIRIKA

Frankfurt, Ujerumani

MWANAMKE mmoja katika mji huu alishangaza jamaa na marafiki kwa kusema kuwa heri mumewe angekufa kuliko mbwa wake.

Duru zinasema mama huyo mwenye umri wa miaka 48 alikuwa akimpenda mbwa huyo sana, lakini hakuna aliyetarajia matamshi kama hayo kutoka kwake.

Mbwa huyo alifariki baada ya kugongwa na gari akivuka barabara. “Juhudi za madaktari wa wanyama katika mji huu kumtibu mbwa huyo hazikufua dafu na akafariki.

Mama huyo alihuzunika mno. Hakuweza kula kwa siku nne. Jamaa na marafiki walijaribu kumfariji lakini hawakufaulu,” mdokezi aliambia jarida www.dogs.com.

Duru zinasema kwamba mumewe anayefanya kazi mji tofautio aliamua kusafiri nyumbani kumtuliza mkewe.

Hata hivyo, mkewe alipomuona alimkemea: “Heri ungekufa wewe kuliko mbwa wangu ambaye alikuwa rafiki yangu mkubwa maishani. Ukiwa mbali, alikuwa karibu nami, nikimuita alikuwa akiitika ilhali wewe huwa unachukua simu zangu unapotaka,” mama alilia mumewe alipojaribu kumkaribia.

Watu walipigwa na butwaa kufuatia matamshi ya mama huyo ambaye hajajaliwa mtoto na wakadhani mumewe angekasirika.

Hata hivyo, jamaa alipiga magoti mbele ya mkewe na kuomba msamaha kisha akaenda kumnunulia mbwa mwingine wa bei ghali ili kumtuliza.

“Watu walidhani jamaa angekasirika kwa kutakiwa kifo lakini walishangaa alipomuomba mkewe msamaha, akatoka na kurudi na mbwa mwingine ambaye bei yake ni mara tatu ya aliyefariki,” mdokezi alisimulia.

Kulingana na mdokezi, mama alipomuona mbwa huyo alifurahi, akamkumbatia na kurudia shughuli zake za kawaida.

“Mpenzi, kama ningekufa, haungepata mbwa mwingine kama huyu,” mumewe alimtania.

You can share this post!

Mudavadi avuna wanachama 350 kutoka Jubilee

Ukosefu wa viwanja vya hadhi unavyoua talanta mitaani

adminleo