Makanga pabaya kwa kutusi kipusa bila kujua ni afande
RUNYENJES, Embu:
MAKANGA mmoja alijikuta pabaya baada ya kudharau kipusa aliyempuuza, akijigamba kuwa haogopi mtu yeyote bila kujua alikuwa akitusi afisa wa polisi.
Inasemekana alimtupia maneno ya kejeli na kumdharau mbele ya wasafiri wengine na kutangaza kuwa hangempeleka popote.
Hata hivyo, mambo yalibadilika ghafla pale kipusa huyo alipotoa simu na kuipiga, hali iliyomfanya makanga azidi kubeza akimwambia aite wapenzi wake wote na hawangemuweza.
Dakika chache baadaye, maafisa kadhaa wa polisi walifika eneo hilo na kumkamata makanga huyo bila mzaha.
Alipogundua alikuwa ametusi afisa wa polisi, makanga huyo alionekana akitokwa na machozi, akijaribu kuomba msamaha lakini alikuwa amechelewa.
Aliishia korokoroni huku wenzake wakisema kiburi chake kilimgharimu uhuru wake.