Lugha, Fasihi na Elimu

Mfano wa yanayoulizwa kwenye ‘Swali la Nne’ mitihani ya Insha

Na SIMON NGIGE, Alliance High School May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

LEO tuangalie swali la nne katika mitihani ya insha. Kimsingi, swali hili huwa ni insha ya kubuni au ya mdokezo.

Mtahiniwa anahitajika kuanza kwa maneno fulani ama kukamilisha kwa maneno teule.

Mtahiniwa anastahili kuzingatia maneno ya mdokezo kikamilifu. Ayafasiri maneno hayo kikamilifu.

Mapambo ya lugha yawepo na kisa kisisimue ajabu. Ubunifu wa hali ya juu usikose. Mitindo mbalimbali ya sentensi itumiwe kiufundi.

Mifano ya maswali hayo ni kama:

  • Andika insha itakayomalizikia kwa: Hapo ndipo nilipotambua kuwa kama masuala yao hayatashughulikiwa kwa dhati, vijana ni bomu ambalo liko tayari kulipuka wakati wowote.
  • Andika insha itakayomalizikia kwa: “Niliipapia ile bilauri ya maji kwa pupa. Sikuwa na uhakika kuwa kiu yangu ingekatika. Nikapiga mafunda mawili, matatu. Baada ya kugugumia bilauri yote, ndipo nilipotambua kuwa kweli maji ni uhai.”
  • Tunga kisa kitakachomalizikia kwa maneno yafuatayo: Nilijaribu kuyafumbua macho yangu yaliyojaa uchovu kutokana na malimbikizi ya usingizi….
  • Tunga kisa kinachoanza kwa maneno yafuatayo: Moyo wangu ulidunda kwa matarajio makuu…
  • Tunga kisa kinachoanza kwa maneno yafuatayo: Mara tu nilipokivuka kizingiti cha lango la nyumba yangu, nilijua kwamba maisha yangu yalikuwa yanachukua mkondo mpya…
  • Tunga kisa kitakachomalizika kwa maneno yafuatayo: Nilimtazama kwa muda. Macho yake yalijaa machozi ya furaha na majonzi…
  • Tunga kisa kitakachomalizika kwa: Niliigugumia ile chupa ya maji kwa pupa. Sikuamini kuwa kiu yangu ingekatika. Baada ya kumaliza kunywa yote, ndipo nilipotambua kwa kweli kuwa maji ni uhai.
  • Tunga kisa kitakachomalizika kwa maneno yafuatayo: Sikuupa moyo wangu nafasi ya kujutia niliyoyatenda. Nilikuwa nimeamua kuyajenga maisha yangu upya.
  • Tunga kisa kinachoanza kwa kauli ifuatayo: “Waja husema kuwa subira huvuta heri: hii yangu inazidi kuvuta machungu kila kuchapo, heri itapatikana lini?’’ Tuama alijisemea kwa masikitiko. Nilimtazama kwa muda. Moyo wangu ulinituma kumuuliza kilichomfanya kuishi katika mazingira ya kudhalilisha kama hayo.
  • Tunga kisa kinachoanza kwa maneno yafuatayo: Msongamano wa wanunuzi, wapitanjia na wasukuma mkokoteni kati mwa wachuuzi wa kila aina ulinitanabaisha kuwa nimefika mji wa Tafaruku.
  • Tunga kisa kinachoanza kwa maneno yafuatayo: “Maskini, anaonekana kuemewa na hisia za kupoteza. Huu mchezo wa bahati nasibu utakuja kutuangamizia kizazi,” akajisemea huku akimtazama mja aliyekuwa kainamia meza huku ameshika kichwa…
  • Tunga kisa kitakachomalizika kwa maneno yafuatayo: Hapo ndipo nilipogundua kwamba mtu akitia bidii kwa jambo hata likiwa gumu vipi hufanikiwa.
  • Tunga kisa kitakachomalizika kwa maneno yafuatayo: Kila ninapokumbuka kisa hicho, ninapata matumaini kwamba maisha yangu yanaweza kubadilika.
  • Tunga kisa kinachoanza kwa maneno yafuatayo: Hakung’amua kitakachotokea. Alichojua ni kwamba hatua hiyo ingemletea afueni.
  • Tunga kisa kinachomalizika kwa maneno yafuatayo: Rafiki yangu alinitazama na bila kusita akaniambia, “Nilikuonya kuwa hapa tusingefaulu.”